Social Icons

Saturday, 26 August 2017

Halmashauri ya Mbozi Yapitia Upya Bajeti yake



Stephano Simbeye, Mbozi

Halmashauri ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe imefanya  mapitio ya bajeti ya 2017/2018 ili kuziba pengo lililotokana na vyanzo vilivyoondolewa na serikali kuu na vingine kupunguzwa viwango.

Uamuzi huo ulifikiwa jana katika kikao maalumu cha baraza la madiwani hao kilichofanyika katika ukumbi wake mjini Vwawa ambapo waliongeza vyanzo kadhaa vipya, kuimarisha vyanzo ambavyo vilikuwepo lakini vilikuwa havikusanywi kwa sababu mbalimbali.

Awali akieleza sababu za mabadiliko hayo Kaimu Mtunza Hazina wa halmashauri ya Mbozi Deodatus Mtaremwa alisema yanatokana na mabadiliko ya sheria ya fedha ya mwaka 2017 ambayo imefuta baadhi ya vyanzo vya mapato vilivyokuwa vinakusanywa na halmashauri na vingine kupunguzwa viwango.

Alisema ushuru wa mazao ya chakula umepunguzwa kutoka asilimia 5 hadi asilimia 2, ushuru wa kahawa umepunguzwa kutoka asilimia 5 hadi 3, pia kuondolewa kwa baadhi ya vyanzo kama ushuru wa mabango, kodi ya majengo vimeathiri bajeti ya halmashauri kwa asilimia 32.

Diwani wa kata ya Halungu Maarifa Mwashitete alisema halmashauri hiyo imekuwa ikitegemea chanzo kimoja cha ushuru wa zao la kahawa na mazao ya chakula huku ikiviacha vyanzo vingine, lakini kutokana na kuteteleka kwa zao hilo wamelazimika kuangalia vyanzo vingine ili halmashauri iweze kujiendesha.

“ Vyanzo vingi vilikuwepo lakini kutokana na uzembe tu vilikuwa havifuatiliwi na vikakusanya ili viingize mapato katika halmashauri jambo ambalo limefanya halmashauri kukosa mapato” alisema Mwashitete

Ili kufanikisha ukusanyaji wa mapato katika chanzo cha mazao watendaji watapaswa kuwatambua wakulima wao ili kuwadhibiti wafanyabiashara wanaotumia mwanya wa kusafirisha mazao yasiyozidi tani moja bila kulipa ushuru kama ilivyoagizwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Pombe Magufuli hivi karibuni.

Bartoni Sinienga ni Diwani toka kata ya Ipunga alipendekeza halmashauri kujenga kiwanda kidogo cha kusindika baadhi ya mazao ili kuongeza thamani na kujipatia mapato, pia alipendekeza vyanzo vingine vinne vipya ambavyo vitasaidia kuongeza mapato ya halmashauri.

Alivitaja vyanzo hivyo kuwa ni pamoja na kuanza kutoza ushuru wauzaji wa mabaki ya vyakula (Pumba) kiasi cha asilimia 2 ya bei, kutoza vibari vya usafirishaji mifugo, mashine za kupukuchua mahindi, kuwatoza mafundi wajenzi wa nyumba, na bidhaa za ngozi kutozwa asilimia 3.

Kwa upande wake Mwanasheria wa halmashauri Deogratus Nchimbi aliwatahadharisha madiwani kuepuka kuingiza vyanzo ambavyo vitakuwa kero kwa wananchi ambapo vinaweza kuongeza tatizo badala ya kutatua tatizo.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Mbozi Erick Ambakisye alisema changamoto ya kukosa mapato ndiyo iliyowafanya waitishe kikao cha dharura ili kujadili na kupitisha mkakati wa bajeti ya mwaka 2017/2016 katika kuongeza mapato ya ndani ya halmashauri na kukusanya kwa asilimia 100.

Alisema wameamua kuweka mkazo wa makusanyo katika vyanzo kadhaa vya ushuru wa madini ambapo Makampuni hayo yalikuwa yanalipa Sh. 1.2milioni kwa mwaka kwa tozo la asilimia 0.02 na kwamba hivi sasa chanzo hicho kitatozwa ada ya Sh. 3000 kwa tani moja itakayosafirishwa madini ya makaa yam awe, marumaru na udongo wa kutengenezea saruji.

Ambakisye alisema ili kufanikisha ukusanyaji wa ushuru wa madini halmashauri yake inatarajia kujenga mzani mpakani mwa wilaya hiyo katika kijiji cha Nanyala ili kupima magari yaliyobeba madini hayo kwa lengo la kupata takwimu sahihi ambapo awali walitegemea takwimu kutoka TMAA.

Mwenyekiti huyo alieleza vyanzo vingine kuwa ni kutoza ada ya uhai wa vikundi ambapo vipo vikundi 700 ambavyo vitalipa Sh. 20000 kila kimoja na kiiingizia mapato halmashauri ya zaidi ya Sh. 140milioni, vikundi zaidi ya 700 vya kuweka na kukopa vitatozwa ada ya mikopo ambayo pia itaipatia halmashauri hiyo zaidi ya Sh. 140milioni,

Aliongeza vyanzo vingine kuwa ni kuyatoza makampuni yanayonunua kahawa wilayani hapa, vikundi vinavyonunua mazao, wafanyabiashara binafsi wanaonunua mazao mchanganyiko na kwamba makusanyo hayo yataipatia halmashauri Sh. 1.55 kwa mwaka kiasi ambacho ni ongezeko la zaidi ya Sh. 800milioni ukilinganisha na makisio ya awali.

Mmoja wa watendaji Rose Vicent aliiomba halmashauri hiyo kuwaongezea nguvu kazi na ulinzi kutokana na ugumu wa kukusanya mapato ambapo mara nyingi kazi hiyo inawafanya wachukiwe na wananchi.

“Ukiwa mtendaji hutakiwi kupendwa na watu lazima uvae sura kavu, tunaomba tupatiwe ushirikiano wa kiusalama kila kata wawepo askari kata ambao watalipwa kutokana na kazi wanayofanya kutokana na asilimia za mgawanyo”alisema

Afisa Tarafa ya Vwawa Haji Hamis Ibrahim alisema upo ugumu katika utekelezaji wa maazimio ambayo madiwani wameyafikia kutokana na wao wenyewe kuingilia utendaji na hasa kuwatetea baadhi ya wananchi wakati wanatozwa ushuru jambo ambalo linakwamisha kazi.

“ mgtakumbuka katika bajeti iliyopita mlikiri kuwa mmeikosea lakini jambo la ajabu ilipofika utekelezaji mkawataka watendaji wajieleze, huku mkisahau kuwa ninyi wenyewe mlikosea tangu mwanzo, hata hivyo watendaji wawezeshwe vitendea kazi ili kufikia malengo” alisema Ibrahim.
Mwisho





No comments:

Post a Comment