Social Icons

Monday, 19 March 2018

Halmashauri Mbozi Kujenga Soko la Mazao Mchanganyiko



Na: Stephano Simbeye MBOZI: 

Halmashauri ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe imetenga zaidi ya Sh. 800 milioni kwa ajili ya kujenga soko la kisasa la mazao mchanganyiko katika mwaka ujao wa fedha ili kuanzisha kituo cha manunuzi cha kuaminika na kutatua kero ya muda mrefu ya wakulima kunyonywa na wachuuzi.

Hayo yameelezwa jana katika kikao cha baraza la Madiwani kilichokutana mjini Vwawa ili kupitisha makisio ya bajeti ya mwaka 2018/2019 kuwa wilaya ya Mbozi ni mzalishaji mkubwa wa mazao ya chakula lakini hakuna soko la uhakika la kuuzia mazao ambalo litasaidia wakulima kuuzia mazao yao huku serikali ikisimamia vipimo halali.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Erick Ambakisye alisema moja ya vipaumbele katika bajeti ijayo ni ujenzi wa soko la kisasa la mazao ambapo zimetengwa zaidi ya Sh. 800milioni ili kujenga soko hilo ambalo aliwataka wataalamu kutafuta eneo zuri litakalofikika kirahisi na watu wote, pia kipaumbele kingine ni kufungua barabara zote zilizoharibika kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha ambapo zimetengwa Sh. 200milioni ambazo zitakabidhiwa kwa wakala wa barabara za mjini na vijijini (TARURA)kwa ajili ya kazi hiyo.

Alisema hatua hiyo imekuja kufuatia soko la awali la mazao lilokuwepo huko nyuma lilijengwa Tunduma lakini baada ya mgawanyo wa wilaya ya Mbozi na Momba na Tunduma kuwa halmashauri ya mji imelazimu Mbozi kufanya mchakato mwingine wa ujenzi wa soko la mazao.

Aidha Ambakisye alibainisha kuwa katika mwaka ujao wa fedha halmashauri yake inatarajia kukusanya zaidi ya Sh. 5.8 bilioni ikiwa ni mapato ya ndani ikiwa ni ongezeko la zaidi ya Sh. 1 bilioni ukilinganisha na bajeti ya mwaka unaoendelea wa 2017/2018 na kuwa katika makusanyo ya mwaka wa fedha wa 2017/18 hadi sasa wamefikia asilimia 54.

Diwani kata ya Nyimbili Tinson Nzunda aliishauri idara ya fedha ya halmashauri kutafuta takwimu halisi za mapato yatokanayo na zao la kahawa na kuacha kutegemea takwimu za watu wengine ambao wamekuwa wakiidanganya na hivyo kusababisha kupata mapato kidogo ukilinganisha na uhalisia wa uzalishaji wa zao hilo.

Diwani wa Halungu Maarifa Mwashitete alisema iwapo watendaji wa halmashauri wakiacha kufanya kazi kwa mazoea watawezesha kufikia mafanikio ya makusanyo ya makisio waliyoyafanya na iwapo ikiwa kinyume chake hapatakuwa na muujiza wa kufikia malengo.

Naye Katibu tawala mkoa wa Songwe anayeshughulikia uwekezaji Halima Mpita aliitaka halmashauri ya Mbozi kuanza kujiendesha kibiashara kwa kuboresha rasilimali zake ili ziweze kuongeza pato ambalo litasaidia kuiongezea mapato na hatimaye kuelekeza kwenye miradi ya maendeleo.

Alitoa mfano baadhi ya vivutio vya utalii ambavyo viko chini ya halmashauri vikiboreshwa vitasaidia kuiingiza mapato, kutumia shamba la serikali la Magamba kuzalisha mbegu na shughuli nyingine nyingi zinzoweza kuongeza mapato yake.

Iwapo uamuzi huu utafanikiwa utakuwa umeunga mkono jitihada za asasi isiyokuwa ya kiserikali ya MIICO ambayo imeanzisha kampeni ya kutaka kuwepo na bei elekezi katika mazao ya chakula itakayozingatia gharama za uzalishaji ili kumkomboa mkulima na kufanya kilimo kiwe na mvuto.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment