Social Icons

Tuesday, 1 November 2016

Polisi Wakamata Mbengu Feki



Na: Stephano Simbeye – Mbozi
JESHI la Polisi mkoani Songwe Kwa kushirikiana na Kampuni ya Mbegu ya Pana jana zilikamata mbegu feki za mahindi aina mbalimbali kiasi cha Kilogramu 455 zenye thamani ya Sh. 3.6milioni katika mamlaka ya mji mdogo wa Mlowo wilayani Mbozi mkoani Songwe.

Kamanda wa Polisi mkoani Songwe Matias Nyange akizungumzia sakata la kukamatwa kwa mbegu hizo Alisema oparesheni ya kuwakamata wafanyabiashara hao wa Mji mdogo wa Mlowo katika Wilaya ya Mbozi ilifanyika Oktoba 30 mwaka huu.

Kufuatia kukamatwa kwa mbegu hizo mkuu wa Mkoa wa Songwe, Luten Mstaafu Chiku Galawa, ametangaza vita kali na wazalishaji na wasambazaji wa pembejeo feki zinazosababisha hasara kwa wakulima katika Mkoa huo.

Galawa aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuwa, serikali mkoani humo haitamvumilia mtu yeyote atakayesambaza mbegu feki , pamoja na pembejeo nyingine ambazo matokeo yake ni kusababisha hasara kwa mkulima.

“Utafiti umeonyesha wazi kuwa suala la pembejeo feki ni tatizo kubwa, kwani utafiti uliofanywa n a watafiti kutoka Chuo kikuu cha Dar es salaam katika  Wilaya za Mbozi na Momba pekee unaonyesha kuwa asilimia zaidi ya 70 ya mbegu na viua tirifu zinazouzwa madukani humo ni feki” alifafanua Galawa.

Aliongeza kuwa, mkoa wa Songwe umejipanga kudhibiti hali hiyo ambapo wakuu wa wilaya na kamati zao wahakikishe wanafanya ukaguzi wa mara kwa mara

Aidha, Galawa alisema serikali Mkoani humo itahakikisha inaongeza udhibiti katika mpaka wa Tunduma kupitia kitengo cha kuthibiti ubora na usalama wa mbegu zinazoingizwa nchini kutoka nje ili kuzuia uingizwaji nchini mbegu feki za mahindi ambazo kwa asilimia kubwa zimekuwa hazina ubora wala usalama.

Kwa upande wake, mkulima kutoka mtaa wa Ichenjezya Kati Pascal Lwila alisema wao kama wakulima hawawezi kutambua mbegu feki bali wanaiomba serikali kwa kuwatumia wataalamu waliopo iongeze juhudi za kudhibiti ili kuwaokoa wakulima wasiangamizwe na wimbi la uuzwaji wa pembejeo feki
Mwisho.

1 comment:

  1. safi sana, tena waendelea kua hvyo hvyo, maana tumechoka kupewa mbengu feki

    ReplyDelete