Social Icons

Wednesday, 7 June 2017

Wakulima wa Mahindi Mbozi na Momba Waanza Kunufaika na mpango wa AGRA



Stephano Simbeye, Mbozi

Mbozi:Vijiji 40 vyenye wakulima zaidi ya 4000,katika wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, vimeanza kunufaika na mafunzo yanayotolewa na wadau wa mnyororo wa thamani wa zao la mahindi (Unyiha Maize Consortium) kupitia mradi wa AGRA – IGGSAS ambapo wameongeza uzalishaji kutoka gunia 8 – 15 kwa hekari moja, hadi kufikia gunia 25 – 35 msimu huu, hivyo kuongeza kipato.

Wakitoa uzoefu walioupata katika mwaka wa kwanza wa kuanza mafunzo hayo ambayo wanayafanya kwa vitendo kupitia mashamba darasa, mkulima kiongozi toka kijiji cha Ipyana Elias Mswima alisema katika kikundi chao walitenga eneo lenye ukubwa wa robo hekari ambapo walipanda mbegu aina mbili tofauti na kutumia mbolea ya kupandia na kukuzia mara tatu na kuwa wamevuna gunia 7.5 sawa na gunia 30 kwa hekari.

Alisema kupitia shamba darasa hilo wakulima walifundishwa mbinu bora za kilimo cha kisasa na chenye kulenga kuongeza uzalishaji na hifadhi ya ardhi, kisha ujuzi huo kwenda kuutumia kwenye mashamba yao hali ambayo imewaongezea pato la mavuno.

Eva Ndawila ni mkulima toka kijiji cha Ihowa alisema zimejitokeza changamoto kadhaa ambazo zimekuwa kikwazo ni kuchelewa kupata pembejeo hali ambayo inawafanya kuchelewa kupanda, alitowa mfano kwamba msimu huu walichelewa kupanda, badala ya kupanda mapema mwezi Novemba walianza kupanda Decemba 26.

Mdau wa mnyororo wa thamani zao la mahindi na mzalishaji wa mbolea toka kampuni ya  Yara Kefasi Sima alisema mabadiliko ya tabia nchi yanawafanya wakulima kushindwa kupanga mipango yao, hivyo kuwashauri kulima kuzingatia hifadhi ardhi na kutumia pembejeo sahihi zenye virutubisho vingi.

Aliwataka waongeze jitihada kuhakikisha shamba linapandwa mimea kwa idadi sahihi isiyopungua 21733 kwa hekari moja kwa nafasi ya sentimeta25 kwa 75,  ambayo ikitunzwa vizuri  watapata mavuno zaidi yanayoweza kufikia gunia 45  hadi 55 badala ya 30 walizopata msimu huu.

Awali akisoma risala mratibu wa mradi wa mnyororo wa thamani wa zao la mahindi Aloyce Kamzora alisema mradi huo unatekelezwa katika wilaya mbili za Mbozi na Momba utagharimu dola za kimarekani 299,568 sawa na zaidi ya Sh. 674.03 milioni za Tanzania katika kipindi cha miaka minne 2016/2020, utawafikia zaidi ya watu 10000 katika vijiji 200.

Alisema katika mafunzo hayo wanawaelimisha wakulima umuhimu wa kutumia pembejeo sahihi katika eneo sahihi, kulima eneo ambalo mkulima anaweza kumudu kulihudumia, badala ya kuwa na shamba kubwa ambalo hawawezi kumudu kuhudumia.

Ofisa kilimo kutoka halmashauri ya Mbozi, Lydia Shonyela aliwataka wakulima hao kuhifadhi vizuri mahindi waliyovuna, na iwapo watahitaji kuuza wayakaushe vizuri kwani kuuza yangali mabichi yataharibu sifa yake na kuwakosesha soko ikigundulika yapo chini ya kiwango kwenye masoko ya ndani na nje ya nchi.

Alisema mafanikio waliyopata yameongeza uzalishaji ukilinganisha na mwaka jana ambapo mavuno yalikuwa tani 212729 na kuwa mwaka huu zitavunwa jumla ya tani 258837

Kuhusu kero ya kuchelewa kupata pembejeo kwa wakati,  Mkuu wa wilaya ya Mbozi John Palingo aliwataka wakulima wilayani hapa kuungana katika ushirika na kutumia mfumo wa stakabadhi gharani kupata mikopo ya kununua pembejeo mapema badala ya kusubiri ruzuku ya  serikali ambayo ni kidogo isiyokidhi mahitaji ya wakulima.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment