Social Icons

Thursday, 31 August 2017

RC Galawa Ataka Bendera Ziondolewe Barabarani



Stephano Simbeye,MBOZI:

Mkuu wa mkoa wa Songwe Chiku Galawa amepiga marufuku upeperushaji wa bendera za vyama na biashara katika hifadhi ya barabara kuu ili kuweka mandhari ya miji katika hali ya usafi.

Kauli hiyo aliitoa jana katika kikao cha wadau wa Afya kilichofanyika mjini Vwawa wilayani Mbozi kuwa shughuli zozote zinazofanyika katika hifadhi ya barabara kuu, ikiwa ni pamoja na bendera za vyama zinazopeperushwa eneo hilo zitoke ili kuacha maeneo hayo safi.

“ Kwakuwa hao wanaofanya biashara zao barabarani wanafuata wateja kwenye vituo vya mabasi, halmashauri zitafute maeneo mengine mazuri nje ya barabara kuu ndiko wajenge stendi na magari yanayochukua na kushusha abiria yaingie huko”alisema Galawa

Kuhusu uchafu unaozagaa kando ya barabarani mkuu huyo wa mkoa aliwaagiza maofisa afya kuanza kuwakumbusha abiria kutotupa hovyo taka wawapo safarini bali watumie vyombo vya kukusanyia taka ambavyo vitakuwa vikitumika ndani ya basi.

 Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo wilayani Mbozi James Mbasha akizungumzia suala la kuondoa bendera barabarani kwa njia ya simu alisema chama chake bado hakijapata taarifa kuhusu zoezi hilo hata hivyo alisema bendera hizo  zina wenyewe walioziweka katika maeneo hayo hivyo ni vizuri akawaita wahusika azungumze nao awambie sababu ya kuziondoa.

“Sisi hatuwezi kuondoa bendera maana hatujui sababu, kwanini anawaogopa wenye bendera awaite akae nao, tunangoja mtendaji yeyote atakayekuja kuziondoa tutamchukulia hatua kwa kumshitaki mahakamani maana zipo kwa mujibu wa sheria” alisema Mbasha.

Akizungumzia kuhusu kuhamisha stendi kando ya barabara Mbasha alisema hilo ni wazo zuri kwani maisha ya watu yapo hatarini kutokana na baadhi ya stendi kuwa barabarani kama ilivyo stendi ya Mlowo ambapo usalama wa watu uko hatarini.

 Afisa Mtendaji wa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlowo Msolomi Dakawa alisema tayari mipango ya kuhamisha stendi imeandaliwa katika eneo jipya la Forest na sasa wanasubiri taratibu za wataalamu wa idara ya ardhi kukamilisha uwekaji wa alama za mipaka baada ya hapo wataingia mikataba na wafanyabiashara ili wajenge vibanda kuzunguka eneo hilo.
Mwisho

No comments:

Post a Comment