Social Icons

Sunday, 31 March 2019

Waziri Mbarawa Awajia Juu Halmashauri ya Momba

Na: Jonasi Simbeye, Chitete


Waziri wa Maji Profesa Makame Mbarawa ameagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuchunguza chanzo cha mgogoro uliyopo  katika mradi wa maji Chitete katika wilayani Momba mkoani Songwe, ambapo halmashauri imevunja mkataba na kumweka mkandarasi mwingine kinyume cha taratibu  na kuchelewesha mradi.

Alisema mradi wa maji Chitete wenye thamani ya Sh.493.2milioni  Umekuwa na mabishano ambayo yanasababisha mradi kuchelewa kukamilika na hivyo kuwafanya wananchi waendelee kukosa huduma ya maji iliyokusudiwa.

“ DC upo hapa naagiza Takukuru waje wafanye uchunguzi wabaini nini kimejificha katika mzozo huo, kama kuna interest za watu tujue na wakati huo tuiombe wakala wa manunuzi (PPRA) watoe ufafanuzi juu ya suala kama hili ili kuondoa ubishani na ili mradi uendelee” alisema Mbarawa

Alisema chanzo cha mabishano hayo ni kufuatia Mkandarasi wa kwanza kuchelewa kufika eneo la kazi ambapo halmashauri ilichukua hatua ya kuvunja mkataba, na kumuweka mkandarasi mwingine   jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu kwa kuwa halmashauri baada ya kuvunja mkataba ilipaswa ipate kibari toka Wizarani kisha taratibu nyingine za manunuzi zingefuata.

Mhandisi wa Maji wilaya ya Momba Maua Mgala alisema chanzo cha mgogoro huo ni mkandarasi kutoonekana eneo la kazi katika kipindi cha miezi mitano tangu alipokabidhiwa kazi, jambo ambalo ni kinyume cha mkataba ambao unaeleza kuwa mkandarasi asipoonekana kwenye eneo la kazi mkataba utavunjwa.

“mkandarasi huyu alisaini mkataba Julai 12 mwaka 2017 lakini hakuonekana hadi Februari 26 mwaka 2018 ambapo ndipo mkataba ulipovunjwa nay eye kujulishwa ndipo alipoleta vifaa vichache na kuandika barua ya kupinga kuvunjwa kwa mkataba”alisema Mgala

Alifafanua kuwa hata hivyo alisema halmashauri ilimvumilia mkandarasi huyo huku ikimwandikia barua za kumkumbusha lakini hakutokea ndipo ilipovunja mkataba na kumchukua mkandarasi aliyeshika nafasi ya pili kwenye zabuni ili aendelee na kazi hiyo.

Kuhusu uamuzi wa Waziri kufuatia sakata hilo Mhandisi Maua alisema ni uamuzi mzuri ambao utatupeleka mahali pazuri na hatimaye kukamilisha mradi ili wananchi waendelee kupata maji.

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Momba Adriano Jungu alimwambia Waziri wa Maji kwamba lilipojitokeza suala la utata wa Mkandarasi huyo alikwenda moja kwa moja Wizarani ili kutoa maelezo ya jinsi hatua mbalimbali alizozichukua kuhusu mkandarasi huyo.

Aidha Kampuni ya DIPE & Company Limited ya Morogoro ndiyo iliyoshinda kandarasi ya kujenga mradi wa maji Chitete wenye thamani ya zaidi ya Sh.493.2 milioni, ambapo wakati wa ziara ya Waziri Mbarawa hakuna mwakilishi wa kampuni hiyo aliyekuwepo.

No comments:

Post a Comment