Social Icons

Thursday, 20 October 2016

Mlowo Yawa Mamlaka ya Mji Mdogo, VIjiji Vyafutwa rasmi



Stephano   Simbeye, Mbozi

MBOZI: Halmashauri ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe imeanzisha rasmi Mamlaka ya mji mdogo wa Mlowo, ikiwa ni njia ya kusogeza karibu huduma kwa wananchi katika mji huo  ambao unakuwa kwa haraka ikiwa na idadi kubwa ya watu.

Afisa mtendaji Mkuu wa Mamlaka hiyo Msoleni Dakawa akizungumza wakati wa kuhitimisha mafunzo ya wenyeviti wa vitongoji ambao wanatarajia kuunda baraza la mji huo na kuhitimisha rasmi mamlaka za serikali za vijiji, alisema mamlaka hiyo imeanzishwa kisheria na ilitakiwa kuanza tangu Julai mosi mwaka huu lakini kutokana na sababu mbalimbali haikuweza kuanza na kuwa hivi sasa inatarajia kuanza baada ya kukamilisha zoezi la kutoa elimu kwa viongozi.

Alisema mara baada ya kuanza litaundwa baraza ambalo litakuwa na mwenyekiti na Makamu wa Mamlaka, pia zitaundwa kamati tatu za kudumu ambazo ni Kamati ya uchumi, ujenzi na mazingira (Huduma za jamii), kamati ya fedha uongozi na mipango miji na kamati ya elimu afya na maji.

“ hata hivyo kwa mujibu wa sharia mamlaka itakuwa na uwezo wa kuunda kamati nyingine mbili kadiri itakavyoona inafaa kulingana na mazingira ya mamlaka ikiwemo kamati ya kudhibiti Ukimwi” alisema Dakawa.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Mbozi Elick Ambakisye aliwataka wajumbe wa mamlaka hiyo kufuata sheria kanuni zilizopo katika kufanikisha majukumu yao lakini pia kuandaa sheria ndogo ambazo hazitakinzana na sheria mama ili kuharakisha maendeleo ya wakazi wa mji wa mlowo.

Alisema Mlowo imekuwa kama kijiji kwa muda mrefu hivyo panahitajika jitihada za makusudi kurejesha tabia ya watu kutofuata taratibu na sheria kwa kufuata taratibu zilizowekwa na zinazotarajiwa kutungwa pia aliwataka wajumbe hao kujitoa Zaidi katika majukumu  waliyokabidhiwa.

Aliwashukuru wajumbe ambao walikuwa wenyeviti wa vijiji kuwa halmashauri inatambua majukumu waliyoyafanya na kuwa mabadiliko haya yamekuja kutokana na mji kukua imelazimu kujipanga upya na kuwa kukua huku kunatarajiwa kuendelea kadiri ya mahitaji.

Mmoja ya wajumbe wa Mamlaka ya mji wa Mlowo Monica Mnkondya alisema mafunzo hayo yamewasaidia kufahamu namna ya uendeshaji wa mamlaka na kwamba yatawasaidia kusimamia shughuli zilizopo mbele yao.

Alisema wamejifunza masuala ya kufuata kanuni sheria na ulinzi na usalama mambo ambayo tangu walipochaguliwa hawakuwahi kuyafanya na hivyo wamekuwa wakifanya kazi bila kujua taratibu zinazopaswa.

Kuanzishwa kwa Mamlaka  ya mji mdogo wa mlowo, kunahitimisha serikali za vijiji ambazo zilikuwa vijiji vinne  vya Mlowo,Nambala, Mbimba na Ivwanga na kuwa kuna  vitongoji 24 ambapo wajumbe wake wanatoka kwenye vyama vya CCM na Chadema kwa idadi sawa ya wajumbe ( CCM 12 na Chadema 12)
Mwisho

No comments:

Post a Comment