Social Icons

Sunday, 30 October 2016

Wakilima Wanaolima Kilimo Hifadhi Mazingira Waanza kunufaika



Na: Stephano Jonasi - Mbozi

Wakulima wa mahindi wanaofanya kilimo hifadhi wameanza kunufaika kwa kuongeza kiwango cha mavuno kutoka gunia 8 walizokuwa wanapata awali kwa ekari moja hadi gunia 25 kwa ekari na hivyo kuanza kuboresha maisha yao.

Wakizungumza jana katika sherehe ya siku ya wakulima iliyofanyika katika kijiji cha Shiwinga wilayani Mbozi mkoani Songwe wakulima hao walisema awali walikuwa hawaamini waliposhauriwa na wataalamu kuanza kulima kilimo hifadhi jambo ambalo hawakuamini.

Bw. Sikujua Msukwa ni mkulima kutoka kijiji cha Nkanga akitoa ushuhuda wake alisema walipopelekwa kwenye mafunzo katika kituo cha utafiti Uyole jijini Mbeya kupatiwa mafunzo ya namna ya kulima kilimo hifadhi hakuweza kuamini na aliendelea kuvumilia ili apate posho waizokuwa wanalipwa tu.

Alisema mara baada ya mafunzo na aliporudi nyumbani wakati wa kufanyia kazi yale waliyojifunza alilazimika kugawa shamba lake katika sehemu mbili ili sehemu moja alime kilimo alichozoea na sehemu nyingine alianza kulima kilimo hifadhi kama alivyofundishwa,  ambapo alipanda siku moja kwa kutumia mbolea na mbegu bora katika sehemu zote mbili.

“ nawaambia ndugu zangu wakati mimea inakuwa nilianza kuona tofauti kati ya eneo lililopandwa kwa kuzingatia kilimo hifadhi na lile lililopandwa kwa kilimo tulichozoea, kwani sehemu niliyolima kilimo hifadhi mimea yake ilikuwa vizuri huku shamba likiwa na unyevunyevu wakati wote tofauti na upande wa pili ambako udongo wake ulikauka muda mwingi” alisema Bw. Msukwa.

Aidha Msukwa alisema mafunzo waliyopata yamewasaidia pia kufanya shughuli za kilimo pasipokumtegemea mtaalamu wa  ugani na kutoa wito kwa wakulima wengine kufika shambani kwake kujifunza kwani wagani ni wachache hivyo wanahitaji kufundishana wenyewe mambo madogo madogo yamsingi katika kilimo chao.

Akisoma risala mbele ya mgeni rasmi mmoja wa wanakikundi cha Maendeleo Shiwinga  ambacho pia kinajihusisha na kilimo hifadhi Bw. Moses Roa  alisema wamefanikiwa kuongeza tija ya uzalishaji ambapo wamekuwa wakilima mazao ya maharage, mahindi na Soya kwa kutumia njia mbalimbali kupitia mashamba darasa  kwa kuonesha matumizi ya mbegu bora na kilimo hifadhi  udongo

Akizungumzia kipato katika zao la maharagwe Bw. Roa alisema katika eneo walilotunza vizuri  walivuna debe 3 ½ na katika maeneo yaliyolimwa kienyeji walivuna debe moja na kuwa maeneo hayo yalikuwa sawa kwa ukubwa wa mita 10 kwa 10

Meneja wa Mradi wa kilimo hifadhi  kanda ya Nyanda za Juu Kusini Bw.  Erastus Mkojera alisema mradi unaendeshwa chini ya usimamizi wa taasisi ya mtandao wa kilimo hifadhi Barani Afrika (CTN) kwa kushirikiana na AGRA, S.N.V, Rucodia, na Pass una lengo la kuhifadhi udongo na kuongeza kipato kwa wakulima.

Akiwahutubia wakulima waliohudhuria sherehe hizo mgeni rasimi ambaye pia ni Ofisa kilimo wilayani Mbozi Bw. Richard Siriri aliwataka wakulima kukimbilia fursa zinazojitokeza badala ya kusubiri ili wanufaike nazo, pia aliwaasa kuitumia siku hiyo kwa kupokea ujumbe waliopata na kuyatumia vizuri mashamba darasa kujifunza tecknolojia inayofundshwa.

Alisema kilimo hifadhi ndicho kitakachoisaidia nchi kuhifadhi udongo kutokana na ukweli kwamba ardhi na maji ndizo rasilimali pekee ambazo haziongezeki lakini kutokana na ongezeko la watu rasilimali hizo zinazidi kupungua siku hadi siku na hivyo zisipohifadhiwa zitapotea na kuleta janga linaloweza kuleta madhara makubwa kwa taifa.

Aidha kilimo hfadhi ni kilimo ambacho wakulima  wanatumia tecknolojia ya madawa pasipo kulima kwa kuvuruga ardhi bali mara baada ya mavuno wanaacha matandazo ya mimea waliyovuna shambani ambapo mvua ikija inaacha unyevunyevu ambao unasaidia kuhifadhi udongo ambapo hakuna udongo unaosombwa na maji tofauti na eneo lililolimwa ambalo linakuwa kame na udongo husombwa na maji ya mvua.
 Mwisho

Na: Stephano Jonasi, Mbozi

Mbunge wa viti maalumu mkoa wa Songwe Bi. Risala Kabongo (Chadema) amesema kukosekana kwa maji katika mkoa wa Songwe wenye mito na vyanzo vingi ni matokeo ya mipango mibovu ya serikali.

Kauli hiyo aliitoa alipozungumza na wakazi wa kitongoji cha Majengo kilichopo katika kata ya Vwawa wilaya ya Mbozi kuwa ni jambo la kushangaza eneo lenye mito, mabonde yanayotililisha maji mwaka mzima halafu wananchi katika eneo hilo wakawa na shida ya maji.

 "Inasikitisha sana wakati neema ya mito  na vyanzo 26 tumepata lakini bado wanawake wanahangaika na kutumia muda mrefu kutafuta maji badala ya kufanya kazi za kuwaongezea kipato" alisema Bi. Kabongo.

 Alisema hajaridhishwa na jinsi serikali inavyoshughulikia changamoto za ukosefu wa maji safi na salama kwa watu wake hata baada ya miaka hamsini ya uhuru kupita.

Mheshimiwa Kabongo aliongeza kuwa serikali ya awamu ya tano inayojinadi kuipeleka nchi kuwa ya viwanda wakati bado maji na mindomvinu ya barabara ni tatizo kubwa huku hatua zinazochukuliwa hazioneshi kutatua haraka changamoto hizo.

 " wananchi pigeni kelele kudai haki yenu ya msingi na mtuunge mkono tinapopiganoa haki zenu, kama ilivyo katika awamu hii ambayo inatuzuia tinapotaka kukutana na wanawake wenzetu" alisema Kabongo.


Aidha Mji wa Vwawa unaokadiriwa kuwa na watu zaidi ya 50000 kwa mujibu ya sensa ya 2012 bado unatumia miundombinu ya maji iliyojengwa miaka ya 1960 wakati mji huu ukiwa kijiji na sasa ni mamlaka ya mji mdogo hivyo kufanya huduma ya maji kutolewa kwa mgawo na wakati fulani kukosekana kabisa.

Mkazi wa eneo la Mtambwe Bw. Livingstone Kibona alisema wamekuwa na shida ya kupata maji ambapo mabomba yaliyopo na waliyounganishiwa kwa bei nzuri hayatoi maji muda mrefu na kusababisha kulazimika kufuata maji umbali mrefu hivyo muda mwingi kupotea bure bila uzalishaji wowote.

Alisema kukosekana kwa maji katika mji huo kumewafanya wanawake  kutumia saa nyingi kutafuta maji na wakati mwingine kuleta migogoro katika ndoa jambo ambalo linarudisha nyuma ustawi wa ndoa zao.

Akizungumzia upungufu wa maji katika mji wa Vwawa mbele ya Madiwani wa Halmashauri ya Mbozi Mhandisi wa maji Bw. Akson Mwasyange aliwashauri madiwani kutafuta fedha ya dharura ili kutafuta chanzo kipya cha maji ambayo yatatengenishwa na taasisi nyingine kama hospitali ili kuongeza upatikanaji wa maji.

Alisema chanzo kilichopo hakina maji ya kutisha hali ambayo inasababisha uhaba muda mwingi na kuleta usumbufu hasa kwa wagonjwa waliolazwa katika hospitali ya serkali ya wilaya (Vwawa)
Mwisho.

No comments:

Post a Comment