Social Icons

Sunday, 9 October 2016

Shule Yakosa Vitabu



 Na: Stephano Simbeye

VWAWA: Shule  ya msingi Ilindi iliyopo kata ya Idiwili wilayani Mbozi mkoani Songwe, haina kitabu hata kimoja  kufuatia uhaba wa vitabu na kufanya walimu  walazimike kuazima kutoka shule jirani ili waweze kufundisha kwa njia ya kuwasomea wanafunzi wakiwa darasni.

Hayo yalisemwa jana na mwalimu mkuu wa shule hiyo Getrude Mwasambili alipokuwa akitoa taarifa kwa Mbunge wa Jimbo la Vwawa Japheti Hasunga kuwa shule hiyo ina uhaba mkubwa wa vifaa vya kujifunzia na kufundishia kama vitabu vya kiada na ziada ambapo wamelazimika kuazima kitabu kimoja kila somo kutoka shule jirani ili walau waweze kutimiza malengo ya muhtasari.

Alisema pia shule hiyo ina upungufu wa miundombinu kama matundu ya vyoo 17, vyumba vya madarasa 8, nyumba 10 za walimu na walimu 7 ambapo hata hivyo wanajitahidi kujipanga kulingana na mazingira yaliyopo ili taaluma isipotee kabisa.

Mwanafunzi Felista Mwazembe alisema hajawahi kuona kitabu shuleni hapo na kuwa walimu wamekuwa wakiwafundisha kwa nadharia na kuandika ubaoni na kwa kutumia karatasi za mitihani zilizotumika katika shule nyingine ambapo wamekuwa wakifanya mitihani hiyo na kufanya usahii ndipo wanajifunza zaidi.

“ mwalimu akiingia darasani anatupatia maelekezo kutoka kitabu alichoshika na kutupa kazi ya kwenda kufanya nyumbani, ambapo tunafundishana sisi wenyewe kupitia makundi”

Kwa upande wake Afisa Elimu kata ya Idiwili Michael Nzunda alisema tatizo hilo limeanza mwaka huu baada ya serikali kusitisha kununua vitabu kutokana na kutaka kuwa na mchapishaji wa aina moja hali ambayo imelit usumbufu mkubwa kwa walimu na wanafunzi.

Akijibu swali kama kwanini wasitumie fedha za ruzuku zinazotolewa hivi sasa na serikali alisema fedha hizo zinakuja na maelekezo maalumu kuwa zitumike katika masuala ya utawala, Michezo, ukarabati na taaluma kwa ajili ya kuandalia mitihani mbalimbali ya majaribio.

Kwa upande wake Mbunge Japheti Hasunga akizungumzia uhaba wa vitabu shuleni hapo alisema  amegundua kuwa shule hiyo ina changamoto nyingi, hata hivyo kuhusu changamoto ya vitabu alisema atajitahidi kutafuta ili walau kupunguza uhaba uliopo ili watoto waweze kusoma na kuwa pasipo vitabu na vitendea kazi vingine haiwezekani kutoa elimu bora.

Sambamba na hilo Mbunge Hasunga ametumia muda huo kuwatahadharisha watu wazima wenye tabia ya kuoa watoto walio chini ya umri wa miaka 18 na kwamba Bunge limepitisha sheria kari za kuwalinda watoto ili wapate nafasi ya kusoma na kutimiza ndoto zao.
Mwisho

No comments:

Post a Comment