Social Icons

Wednesday, 21 December 2016

Amkataa Mtumishi hadhaani



Stephano Simbeye , Mbozi

VWAWA: Mkuu wa mkoa wa Songwe Luteni Mstaafu Chiku Galawa amemfukuza katika mkoa wake Ofisa Mazingira wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Hamisi Nzunda baada ya kushindwa kutekeleza agizo lake la kufanya usafi kila jumamosi na kutokuwa na mpango kazi unaeleweka wa kufanya miji kuwa safi.

Hayo yalijitokeza jana alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa halmashauri hiyo wakati wa kuhitimisha ziara yake ya siku mbili wilayani hapa ambapo  alikuwa anawaita wakuu wa idara mmoja baada ya mwingine akitaka kupata taarifa zao za utendaji kazi, lakini ilipofika zamu ya ofisa huyo alishindwa kueleza mikakati aliyo nayo katika kuweka miji ya Mlowo na Vwawa katika hali ya usafi.

Mkuu huyo wa mkoa alimuuliza ofisa huyo wa mazingira namna agizo lake la kufanya usafi wa jumla kila Jumamosi, ikiwemo na utekelezaji wa agizo la Rais la kufanya usafi kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi ambapo katika majibu yake alikiri kuwa tangu atoe agizo hilo limetekelezwa mara mbili tu jambo lililomkasilisha Galawa.

  wewe hunifai kufanya kazi na mimi sikutaki ndani ya mkoa huu, unachukua mshahara bila kufanya kazi, tangu nitoe maagizo ya kuwataka kufanya usafi wa jumla kila jumamosi mmefanya mara mbili tu mnataka Mkuu wa mkoa aje ndipo mfanye asipokuwepo hamfanyi” alisema Galawa kwa kufoka

Alisema kuna majanga ya moto yanatokea katika maeneo ya hifadhi lakini hakuna hatua zozote zinazochukuliwa, pia kuna mtu amejenga juu ya kilima aliagiza aondolewe lakini hakuna hatua zilizochukuliwa huku ujenzi katika maeneo ya hifadhi ya misitu ukiendelea.

Awali akitoa majibu yake kwa mkuu wa mkoa ofisa mazingira huyo Hamisi Nzunda alikiri kutotekeleza maagizo ya kufanya usafi kila jumamozi kutokana na uchakavu wa magari ya kusombea taka kuwa halmashauri ina gari moja na trekta moja ambayo yote ni machakavu, hivyo kutokidhi mahitaji ambapo taka zinazozalishwa katika miji hiyo ni nyingi zinazokadiliwa kufikia zaidi ya tani 18 kwa siku.

Alisema katika kutatua tatizo hilo halmashauri imetenga zaidi ya Sh. 88milioni kwa ajili ya kununua trekta lenye matela mawili kwa ajili ya kazi hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa halmashuri ya Mbozi Edina Mwaigomole alisema halmashauri yake imeandaa sheria ndogo inayowataka wazalishaji wa taka kuchangia gharama za kuzoa taka ili kuondoa mlundikano wa taka katika miji.

Alisema katika mpango huo wanatarajia kuwatumia vijana wenye pikipiki za magurudumu matatu ambao watapita kila mtaa kukusanya taka majumbani na kwenda kuzitupa kweny dampo na kuwa mpango huu pia utatoa ajira kwa vijana ambao watalipwa asilimia 70 ya makusanyo ya fedha ya uchagiaji.

Hata hivyo suala la usafi liliibuka pia katika mkutano wa hadhara kwenye mji mdogo wa Mlowo ambapo mkazi wa mji huo Mawazo Mdolo alisema serikali ihamishe ghuba lililopo karibu na makazi ya watu kutokana na mlundikano wa taka ambao unatishia afya za wakazi wa eneo hilo.

Alisema wamekuwa wakifuatilia suala hilo katika mamlaka ya mji huo lakini majibu wanayopatiwa hayawaridhishi hivyo kuona kama serikali haijali afya zao na watoto wao ambao wanaweza kushambuliwa na magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu na kuhara.

No comments:

Post a Comment