Social Icons

Wednesday, 21 December 2016

RC: Galawa Aitaka Halmashauri Mbozi Kuwakopesha Vijana Wanawake Ifikapo Februari 2017



Stephano Simbeye, Mwananchi
Vwawa: Mkuu wa mkoa wa Songwe Luteni Mstaafu Chiku Galawa ameujia juu uongozi wa hamashauri ya Mbozi kufuatia kushindwa kutoa mikopo kwa vijana na wanawake kama ilivyoagizwa na serikali, kuzitaka halmashauri kutenga asilimia 10 ya mapato yake kwa ajili ya kuvikopesha vikundi hivyo badala yake imezielekeza fedha hizo kwenye matumizi mengine.

Hayo  yanafuatia malalamiko ya mkazi wa Vwawa Said Adamu ambaye aliuliza swali katika mkutano wa hadhara akidai serikali ilitoa ahadi ya kukopesha mikopo yenye masharti nafuu kwa vijana na wanawake lakini mikopo hiyo hawaioni na kudai apewe maelezo kikwazo ni nini.

Katika majibu yake Ofisa Maendeleo ya jamii Msolini Dakawa alisema mikopo imeendelea kutolewa licha ya kuwa ni kidogo ambapo hadi sasa zaidi ya Sh. 39 milioni zimekopeshwa katika nusu ya mwaka huu wa fedha na kuwa kazi hiyo inaendelea kadiri fedha zinavyopatikana.

Akifafanua zaidi Dakawa alisema fedha hizo zimetolewa kwa vikundi 20 vya wanawake na 10 vya vijana ambapo imeidhinishwa wiki iliyopita na kamati ya mikopo.    

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya Edina Mwaigomole akitoa ufafanuzi alisema halmashauri yake imeshindwa kutekeleza agizo hilo kutokana na kutingwa na kazi za utengenezaji wa madawati atika msimu uliopita na kuwa fedha hizo zitatolewa katika kipindi hiki kinachoendelea.

Alisema halmashauri katika nusu ya mwaka wa fedha uliopita imekusanya zaidi ya Sh. 1.5 bilioni ambapo ilistahili kuwa iwe imetoa mikopo kwa makundi ya vijana na wanawake zaidi ya Sh. 150 milioni lakini haikufanikiwa kutokana na changamoto ya mwingiliano wa majukumu.

Hata hivyo sababu hizo hazikumridhisha mkuu huyo wa mkoa ambapo alikuja juu na kuanza kutoa maelekezo kwamba kushindwa kutoa fedha hizo kwa makundi husika ni sawa na kutengeneza bomu kwa serikali ambalo litaleta tatizo baadaye na kuwa ni kuwadhuumu wanyonge haki yao ya msingi.

“ serikali ilipoweka utaratibu huo ilijuwa kuwa halmashauri zina majukumu mengi lakini mnashindwa kufanikisha haya kutokana na uzembe wenu wa kushindwa kukusanya mapato ya ndani lakini kama mungekuwa mnaumiza vichwa kutafuta mapato haya yasingewasumbua” aisema Mkuu huyo wa mkoa

Galawa alitumia muda huo kuiagiza halmashauri kuhakikisha inakamilisha kutoa mikopo iliyosalia ifikapo mwezi februari mwaka ujao na taarifa aipate mapema ofisini kwake.

Sambamba na hilo mkuu huyo wa mkoa aliwataka wataalamu wote wa idara ya maendeleo ya jamii kuhamia katika vijiji ambako ndiko kwenye watu ili wakawaelimishe namna ya kutumia mikopo hiyo ili iweze kutumika kama mbegu ambapo ikiota waweze kurejesha na wengine wakopeshwe.
mwisho

No comments:

Post a Comment