Social Icons

Tuesday, 27 December 2016

Mkuu wa mkoa Songwe Akagua Mpaka wa Tanzania na Zambia - Atoa maagizo Mazito




Stephano Simbeye - TUNDUMA:

 Mkuu wa mkoa wa Songwe Luteni Mstafu Chiku Galawa ametoa siku saba kuanzia jana kwa  wafanyabiashara  wanaoendesha shughuli zao kwenye eneo la mpaka  kati ya Tanzania na Zambia mjini Tunduma wilayan Momba, kuhama katika eneo hilo na kuhamia maeneo mengine yaliyotengwa na halmashauri ya mji huo.

Kauli hiyo aliitoa jana wakati alipofanya ziara kukagua mpaka huo ambao  umevamiwa na wafanyabiashara katika eneo hilo ambalo halipaswi kufanywa shughuli yoyote mita 50 kutoka kwenye jiwe la mpaka kila upande na kueleza kuwa serikali imetenga maeneo kadhaa ya kufanyia biashara ili watu wake wasivunje sheria za kimataifa zinazolinda mpaka huo.

Aliwaambia baadhi ya wafanyabiashara hao kuondoa kila kitu na kuacha mpaka wazi katika umbali unaokubalika na kuachana kuendesha shughuli zao kwa kiholela jambo ambalo linaleta sura mbaya kwa nchi jirani ya Zambia na nchi nyingine zilizo Kusini mwa Afrika kutoakana na kuwa mpaka wa Tunduma ni mapokezi ya wageni wanaoingia nchini Tanzania.

Galawa alisema kitendo cha wafanyabiashara hao kukaa karibu ya mpaka kinatowa mwanya kwa watu wenaopitisha mizigo ya magendo kuingia nchini bila kujulikana hali ambayo pamoja na kuikosesha serikali mapato lakini pia inafanya mpaka huo kuwa holela kwa watu wake kutofuata taratibu na hivyo kuwataka kubadilika na kuondokana na mazoea waliyokuwa nayo.

“ hebu angalieni wenzenu nchi jirani kattika eneo lao la wazi wamelitunza na kupanda miti hali ambayo inalifanya lipendeze, lakini huku kwetu lipo kiholela jambo ambalo linaleta sura mbaya hivyo shughuli hizi za magereji, uegeshaji magari, maaduka wakiwemo wauza mazao na mkaa sitaki kuwaona hapa baada ya muda huo kupita name nitakuwa nikipita kila wiki na wewe DC hakikisha utekelezaji wa agizo langu” alisema Galawa

Mmoja wa wafanyabiashara aliyekutwa eneo hilo ambaye anatoka upande wa Zambia Joel Siame alisema eneo hilo amekuwa akilimiliki miaka mingi lakini kwa kutambua kuwa lipo katika mpaka aliandika barua ofisi ya Mkurugenzi wa Tunduma ili aweze kupimiwa aweze kuendeleza shughuli zake kihalali.

Braight Ngwila mkazi wa Nakonde alimwambia mkuu huyo wa mkoa kuwa wamekuwa wakilitumia eneo hilo kama viwanja vya michezo na kuwa viongozi wa pande zote akiwemo mwalimu Julius Nyerere waliwataka kulitunza pasipo kufanya shughuli nyingine bali liwe eneo la amani.

Alisema katika kipindi kirefu wamekuwa wakiishi kama ndugu kwa kushirikiana katika mambo mbalimbali hivyo si vizuri wakaanza kugombana kwa ajili ya eneo ambalo waasisi wan chi hizo waliagiza liwe la amani.

Mmoja wa wafanyabiashara katika eneo hilo Beaty Mwasyeba aliomba serikali kuwapa muda zaidi ili waweze kuhama katika eneo hilo ombi ambalo hata hivyo lilikataliwa na mkuu huyo wa mkoa kwa madai kuwa wapo katika eneo hilo kwa kuvunja sheria hivyo waharifu hawawezi kupewa muda zaidi ili waendelee kufanya uovu.

Mwasyeba alisema wanalazimika kuwepo katika eneo hilo ili kuwa karibu na wateja ambao wengi wanatoka nchini Zambia na kuwa hawawezi kufika kwenye maeneo mengine kwa kuhofia kuvunja sheria.

Rose Damsoni alisema kitendo cha wafanyabiashara wengine kukaa katika maeneo yasiyo rasmi kinawafanya walioko kwenye masoko maalumu kukosa wateja lakini iwapo kila mmoja akatimiza wajibu wake kwa kuhamia eneo rasmi hali itabadilika.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Mji wa Tunduma Valery Kwembe alisema halmashauri imetenga maeneo mawili katika soko la kimataifa ambako wafanyabiashara hao walipewa na kujenga vibanda zaidi ya 2000 lakini hawataki kwenda kulitumia eneo hilo na eneo linginne limetengwa katika eneo la Kaloleni kwa ajili hiyo.

Aidha alisema yeye pamoja na timu yake siku ya kesho (jana) watakwenda kuwaonesha wale wote ambao hawajapata eneo la kuweka vibanda vyao ili waweze kuendesha biashara zao.

Hata hivyo katika eneo la mpaka wa Tunduma ambalo limekuwa likikuwa kwa kasi limejengwa kiholela, hali inayofanya baadhi ya watu kujenga kwenye eneo la wazi la mpaka huku upande mmoja wa nyumba ukiwa Tanzania na upande mwingine ukiwa Zambia hali inayofanya hali ya ulinzi hasa udhibiti wa biashara za magendo kuwa mgumu.
mwisho


No comments:

Post a Comment