Social Icons

Friday, 23 December 2016

Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Songwe Kujengwa Nselewa, Manispaa ya Mbozi yaanzishwa




Stephano Simbeye, Mbozi

Kamati ya Ushauri ya mkoa wa Songwe imeridhia ofisi za mkuu wa mkoa kujengwa katika kijiji cha Nselewa kilichopo kata ya Mlowo wilaya ya Mbozi na kuazimia kuuanzisha Manispaa ya Mbozi  na halmashauri ya Mbozi.

Suala la wapi zijengwe ofisi za mkuu wa mkoa limekuwa likijadiliwa na watu wa lika mbalimbali tangu kuanzishwa mkoa, hivyo kuwapo kwa makundi yanayovutana kila moja likivutia upande  wake, lakini pia makundi hayo yakijihusisha na Siasa, hivyo kufanya kuwa ajenda ya kuzungumzwa kila mahali.

Hata hivyo jana katika kikao cha kamati ya ushauri ya mkoa (RCC) ili kupata eneo la kujenga ofisi hizo,wajumbe walizingatia vigezo kama vilivyoainisha na wataaamu ambapo maeneo hayo mawili yalilingana vigezo hali iliyofanya uamuzi kupatikana kwa kupiga kura na eneo la Nselewa kupata kura nyingi huku eneo la Hasamba likipata kura moja.

Akiwasilisha azimio la kamati ya ushauri ya wilaya ya Mbozi (DCC) mkurugenzi wa halmashauri Edina  Mwaigomole alisema kamati hiyo iliazimia kuwa ofisi ya mkuu wa mkoa ijengwe katika eneo la Hasamba kutokana na eneo hilo kuwa tulivu kwa kuwepo ikulu ndogo, pia fidia ya mashamba ni kidogo na kuwa eneo la Nselewa halifai kutokana na kuwa karibu na barabara na shughuli za watu, hivyo linaweza kusongwa na watu na pia fidia ya mashamba ya watu ni kubwa.

Akizungumzia  uundaji wa Manispaa ya Mbozi na halmashauri ya Mbozi mkurugenzi huyo alisema kamati ilipendekeza manispaa kuundwa na kata 18, huku halmashauri ikibaki kuwa na kata 22 zenye vijiji 101 na vitongoji 540 na kuwa Manispaa itakuwa na idadi ya watu 140000.

Mwenyekiti wa halmashauri ya Tunduma Ally Mwafongo akijadili alisema ni vizuri ofisi za mkuu wa mkoa zijengwe Nselewa ili kuleta madhari nzuri ya mkoa kwa vile eneo hilo lipo katika mwiinuko na kuwa patapendeza zaidi na kuwa mapendekezo ya kuunda manispaa yabaki jinsi yalivyo.

Mbunge wa Jimbo la Vwawa Japheti Hasunga alisema iwapo uamuzi utatolewa kujenga ofisi za mkuu wa mkoa eneo la Nselewa ni eneo ambalo kutokana na kuwa jirani na makazi, shughuli za watu na kuwapo na barabara kuu ya Tunduma – Dar es salaam patasongwa muda mfupi na hivyo kuleta usumbufu.

Alisema sababu ya kupendekeza eneo la Hasamba pajengwe ofisi hiizo ni kuwa eneo hilo ni tulivu kwa staha ya kimkoa, kiusalama na kuwa panafaa hata kujenga Ikulu ndogo kwa ajili ya kupumzikia Rais ukilinaganisha na Nselewa.

Hasunga aliongeza kuwa eneo la Hasamba halihitaji kuwafidia watu kwani ni la serikali ambalo lilikuwa linamilikiwa na walowezi na baadaye kuchukuliwa na serikali ambayo ililikodisha kwa wananchi , lakini pia litarahisisha mawasiliano kati ya wilaya ya Ileje na makao makuu ya mkoa na pia wakati wa Kampeni za uchaguzi Rais aliwaahidi wananchi  kuwajengea barabara yenye urefu wa kilometa 7 kuelekea eneo hilo

Mbunge wa Jimbo la Mbozi Pascal Haonga alipendekeza Nselewa ili kuunganisha miji ya Mlowo na Vwawa kuwa Manispaa moja pia wageni wataweza kuona kitu kipya na kuwa sababu zozote zinazotolewa hazina msingi wowote.

Awali Mwenyekiti wa kikao hicho mkuu wa mkoa Songwe Chiku Galawa aliwaeleza wajumbe kuwa taasisi za mkoa zinapaswa kusambazwa katika maeneo tofauti ili kusambaza huduma kwa jamii na kuwa huduma kama hospitali ya rufaa ya mkoa, Chuo kikuu, Uwanja uwanja wa michezo, VETA na taasisi nyingine zitaekwa katika maeneo mengine ndani ya manispaa ya Mbozi.

Alisema wazo la kujenga taasisi zote katika eneo moja halitafaa kwa sasa bali zitasambazwa ili kila mwananchi aguswe.

Kwa upande wa wananchi wakazi wa mji wa Vwawa baada ya kupata taarifa za kuteuliwa kwa eneo hilo walitaharuki huku wakiwa katika makundi wakijadili suala hilo kwa masikitikiko huku wenzao wa eneo la Mlowo wakipokea taarifa hizo kwa furaha na shangwe.

Nivard Lwila ni mkazi wa Vwawa alisema inasikitisha kuona kuwa ahadi ya Rais  na aziri mkuu wa awamu ya nne waliyoitoa wakati alipofika kuomba kura imepuuzwa ambapo pia aliahidi kujenga kilometa 10 za barabara ya lami kuelekea eneo la hasamba lilikopendekezwa kujengwa ofisi za mkuu wa mkoa.

“sasa mji wa Vwawa unazidi kumalizwa nadhani hatuna wawakilishi maana wameshindwa kutetea mapendekezo ya awali”alisema Lwila

Naye Sailas Kayuni mkazi wa Mlowo alisema kilichotokea ni ushindi ambao unatokana na viongozi wao kuwa mahili wa kuwasilisha hoja.

Aidha awali maeneo matatu ndiyo yaliyopendekezwa kujenga ofisi za mkuu wa mkoa ambayo ni pamoja na eneo la Oldvwawa, Mbimba Tacri na Hasamba na baadaye kuongezwa eneo la Nselewa ambalo halikuwepo kwenye mapendekezo ya awali.

Hata hivyo maeneo yote manne  yaliyopendekezwa yalifanyiwa utafiti na wataalamu ambapo maeneo mawili ndiyo yaliyokidhi vigezo ikiwemo uwezo wa udongo kuhimili kujengwa majengo marefu ikiwa ni eneo la Nselewa na Hasamba.
Mwisho.



No comments:

Post a Comment