Social Icons

Sunday, 1 January 2017

Askofu K.K.K.T Ahimiza wananchi kufanya usafi




Na: Danny Tweve - Mlowo

ASKOFU wa Kanisa la KKKT DAYOSISI YA KONDE DR ISRAEL PETER MWAKYOLILE amesema kuna haja kubwa kwa wananchi wa Tanzania kuunga mkono jitihada za  Rais John Pombe Magufuli anazozifanya katika kusafisha serikali yake na wananchi pia kuwa sehemu hiyo ya usafi.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha zoezi la usafi wa mazingira katika mji mdogo wa Mlowo wilayani Mbozi mkoa wa Songwe ambako alikuwa mgeni rasmi askofu Mwakyolile alisema, wakati Magufuli akisimamia usafi na uadilifu wa watendaji wa serikali, wananchi nao wanapaswa kuwa wasafi tangu kwenye kaya zao, maeneo yao ya biashara na mazingira wanayoyazunguka ili kwa pamoja kuifanya nchi kuwa edeni njema.

Alisema wakati Mungu akiwaweka watu wake kwenye bustani ya Edeni, alitarajia kuwa wangeyafaidi mema ya bustani hiyo lakini kwa bahati mbaya ushawishi wa shetani uliwapotosha watu wale sawa na sasa ambapo nchi zetu zimekuwa na kila namna ya fursa na utajirj lakini baadhi ya watu wametumia vibaya fursa hizo kwa kujinufaisha binafsi.

 Akizungumzia zoezi la usafi wa mazingira, Askofu Mwakyolile alisema kuwa wakati huu tunapoingia kwenye kipindi cha masika, ni dhahiri kutajitokeza milipuko ya magonjwa hasa kipindupindu hivyo ni vyema wananchi wakajielekeza kuhakikisha kuwa wanajali usafi kwenye maeneo yao.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Mbozi John Palingo alisema hatua ya kushirikisha viongozi wa kiroho kwenye kampeni za usafi inalenga kuongeza ushiriki wa wananchi kwenye jukumu hilo hasa kutokana na ukweli kwamba viongozi hao wamekuwa na ushawishi mkubwa kwa waumini wao.

 Alisema eneo la Mlowo ni miongoni mwa maeneo ya kimkakati katika masuala ya usafi wa mazingira na kwamba kupitia utaratibu wa usafi kila Jumamosi, wananchi watakuwa wakijisimamia wenyewe kwenye maeneo yao na hivyo kupunguza uwezekano wa kukumbwa na magonjwa ya mlipuko kutokana na uchafu.

 Zoezi hilo limehusisha wananchi, wafanyabiashara, viongozi wa ngazi mbalimbali na waendesha bodaboda ambapo watu wanaokaidi maelekezo pia walitozwa faini za papo kwa papo kiasi cha shilingi 50,000/=kwa kaya
Mwisho.

No comments:

Post a Comment