Social Icons

Monday, 9 January 2017

Watakiwa Kujiunga Pamoja uimarisha Uchumi


Na: Bershaza Mwabenga, Mbozi



Wananchi mkoani Songwe wametakiwa kujiunga katika vikundi vya ujasiriamali ili kupunguza changamoto mbalimbali za kimaisha na ukali wa maisha kuliko kufanya shughuli za kiuchumi wakiwa mtu mmoja mmoja.

Wito huo umetolewa na mwenyekiti wa kikundi cha mshikamano Meshack Mwambogolo wakati wa maadhimisho ya mwaka mmoja ya kikundi hicho yaliyoambatana na zoezi la upandaji miti 300 katika shule za msingi Mlowo Na Itete zilizopo katika kata ya Mlowo wilayani Mbozi mkoani Songwe.

Mwambogolo alisema kuwa wananchi wanatakiwa kujitokeza kujiunga katika vikundi ikiwemo kujiunga na kikundi cha mshikamano ili kiweze kusajiliwa kama saccos kuliko kubaki kama kikundi cha ujasiaramali ambacho idadi ya wananchama ni chache hivyo ili kuwa saccos ni vyema watu wakajitokeza kujiunga na kikundi hicho.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuadhimisha mwaka mmoja wa kikundi hicho mzee Alan Mwampamba alisema kuwa wanakikundi hicho wanatakiwa kushikamana kwa pamoja kuliko kuwa na vikundi vya mpito ambavyo havina mwendelezo na wasikubali kamwe kuruhusu mianya ya migogoro ambayo itawafanya kupunguza mshikamano na umoja ndani ya kikundi. 

Naye mshauri kutoka ofisi ya ushirika mkoani Songwe Fredy Katundu alisema kuwa kikundi hicho kiwe mfano kwa vikundi vingine ambavyo vimewahi kuanzishwa na kuishia kuwa na dhuluma kwa wanachama huku viongozi wa vikundi wakiwa na jeuri ya kutofikishwa mahakamani kwa kukosa ushahidi hali iliyochangia wilaya kushindwa kukopesheka na taasisi za kifedha.

Kwa upande wake mgeni rasimi mkuu wa wilaya ya Mbozi John Palingo akimwakilisha mkuu wa mkoa wa Songwe alisema kuwa ushirika ndiyo njia pekee ya kumkomboa mwananchi wa hali ya chini na kumuinua kiuchumi.

Aidha Palingo aliongeza kuwa kikundi hicho kinahitaji kuongeza wanachama ili kiwe saccos na kuwa wao kama halimashauri wako katika hatua za kuunganisha vyama viwili vya ushirika ili waunde chama kimoja cha ushirika kilicho na nguvu kutokana na kuwa vyama vingi vya ushirika havikopesheki kwa kukosa viongozi walio na maadili.

No comments:

Post a Comment