Social Icons

Saturday, 18 February 2017

MADAI YA WALIMU KWA SERIKALI YAWAPUNGUZIA ARI YA KAZI




 Na: Stephano Simbeye, Mbozi

Serikali imeshauriwa kutatua kero mbalimbali zinazowakabili walimu ikiwemo kuwalipa madeni yao sambamba na kuboresha miundombinu ya kutolea elimu ili kuongeza ufaulu.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu wa chama cha walimu Tanzania (CWT) mkoa wa Songwe Emelia Mwakyoma wakati akijadili matokeo mabaya ya mitihani ya darasa la saba na kidato cha nne mwaka jana ambapo mkoa wa Songwe ulishika mkia, kuwa wakati zinatizamwa changamoto zilizochangia matokeo mabaya pia litazamwe suala la walimu kutolipwa stahiki zao ambalo linawafanya washindwe kufanya kazi kwa ari.

Katika kikao hicho ambacho kilifanyika katika shule ya sekondari Vwawa wilayani Mbozi mkoani hapa, Mwakyoma alisema kuwa sababu nyingine ni utoro wa walimu kutofanya kazi ingawa wanafika shuleni lakini hawafundishi hatua ambayo usimamizi thabiti unatakiwa ili kuidhibiti

Mkaguzi na mdhibiti wa elimu wilayani Mbozi Jackson Lwafu  alisema kudorora elimu kunatokana na wakurugenzi wa halmashauri kutotekeleza ushauri wanaopewa na wataalamu wa ubora wa elimu ambao hutolewa baada ya ukaguzi na kubaini mapungufu  huwa haufanyiwi kazi hasa katika shule za serikali.

 Alisema baadhi ya kasoro wanazobainisha katika ukaguzi ambazo pia huwa wanashauri wakurugenzi wa halmashauri ni pamoja na uwiano mbovu wa ikama ya walimu ambapo kuna shule zinakuwa na walimu wengi hasa za mjini, wakati zingine zina uhaba, mrundikano wa watoto madarasani, baadhi ya walimu kutofundisha ingawa wanafika kazini, usimamizi mbovu na kukosekana ufuatiliaji.

"Yote mapungufu haya tumekuwa tukitowa taarifa lakini hayafanyiwi kazi hasa kwa shule za serikali, na mahala pengine tinalazimika kuamuru mwalimu arudie kufundisha somo husika, na pengine tunashauri walimu wakuu waliopo wavuliwe madaraka kutokana na udhaifu katika usimamizi lakini yote hayafanyiwi kazi"alisema Lwafu.

Charles Chenza mi mmoja ya wadau akichangia mawazo yake alisema kuna upungufu wa viwango vya vipimo vya malengo ya kuongeza ufaulu, na kuwa mbali ya changamoto ya miundombinu kuna mapungufu ya mahudhurio kwa wanafunzi na walimu.

Alisema ni vizuri ikawekwa mikakati na alama za ufaulu wa kujipima ambazo lazima kila mwanafunzi azifikie, harafu usimamizi uimarishwe ili kuhakikisha walimu wanahudhuria kufundisha, lakini pia nao wanafunzi wanahudhuria ili kupata mtiririko mzuri wa masomo.

 Naye mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya Momba Adriano Jungu alisema wilaya yake ambayo imekuwa ya mwisho kati ya halmashauri tano za mkoa huo inakabiliwa na tatizo la utoro kutokana na jamii ya wafugaji kuhamahama na umasikini ambapo baadhi ya wazazi wanawatumia watoto ambao ni wanafunzi kufanya vibarua ili kupata chakula.

Alitowa mfano mwaka jana ambapo   wanafunzi zaidi ya 800 walisajiliwa kidato cha nne lakini waliojitokeza kufanya mtihani ni wanafunzi 300, hata hivyo ili kukomesha tabia ya utoro wameamua kuanzisha mahakama inayotembea (mobile court) kuwasaka wazazi wenye watoto watoro na kuwahukumu papo hapo.

Akitoa takwimu za ufaulu mwaka 2016 kaimu ofisa elimu mkoa wa songwe Samweli Mshana alisema mkoa una jumla ya shule za msingi 404 zikiwemo 397 za serikali na 7 ni za binafsi  na shule za sekondari ni 104 zikiwemo 82 za serikli na 22 za watu binafsi.
Alisema katika matokeo ya kumaliza darasa la saba mwaka jana mkoa wa Songwe ulishika mkia kitaifa na katika matokeo ya kidato cha nne ya mwaka jana mkoa ulishika nafasi ya 20 kitaifa matokeo ambayo bado hayaridhishi.

Aidha akifungua kikao hicho mkuu wa mkoa wa Songwe Chiku Galawa alipiga marufuku walimu wakuu kuja wilayani kupata huduma mbalimbali za kiofisi badala yake aliwataka wakurugenzi na maofisa elimu kupanga ratiba ya kutembelea vijijini na kujionea wenyewe hali ya shule zao na kuwatatulia walimu matatizo yao kwa kufanya hivyo walimu hao watapata muda mzuri wa kusimamia shule na kufundisha.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment