Social Icons

Sunday, 5 February 2017

Zao la Kahawa lafifisha Ucumi Mbozi



Stephano Simbeye, Mwananchi
ssimbeye@mwananchi.co.tz
MBOZI:Zao la kahawa ambalo miaka ya nyuma lilipata umaarufu mkubwa wilayani Mbozi,mkoani Songwe limeanza kupoteza umaarufu, huku vijana wakisusa kujishughulisha nalo, badala yake wakulima wamejiingiza zaidi kulima mahindi na mazao mengine ya nafaka

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wakulima, walisema kuwa zao hilo limepoteza mvuto kiuchumi kutokana na kukabiliwa na matatizo mengi likiwemo soko la uhakika,magonjwa na ukame,  hali ambayo imekuwa chanzo cha kuwarudisha nyuma badala  ya kuwainua kiuchumi.

Laurent Mgala ni mkulima toka  kijiji cha Ibembwa alisema zao la kahawa linakabiliwa na magonjwa matatu makubwa ambayo yamekuwa kikwazo katika uzalishaji nayo ni pamoja na ugonjwa wa mizizi ambao unakausha mibuni,  Chulebuni na kutu ya majani na kuwa magonjwa hayo yanarudisha nyuma jitihada zao.

Alisema mbali na magonjwa hayo pia kuna mdudu ambaye amekuwa akitoboa mibuni na kufanya ikauke, jambo jingine ni mabadiliko ya tabia nchi ambayo yanafanya ukame wa muda mrefu ambapo zao hilo linahitaji maji mengi wakati wa kuchavusha, kukomaza punje na hata wakati wa kuchakata, lakini kutokana na ukame wanakosa maji ya kumwagilia kwa kukosa mabwawa.

Amosi Kibona mmoja wa vijana alisema ni vigumu kwa vijana kujiingiza kwenye kilimo cha kahawa kwa kuwa hakilipi, bali wanaweza kufanya biashara ya kununua na kuuza kahawa badala ya kulima pia zao hilo linahitaji uwekezaji wa muda mrefu tofauti na mazao ya nafaka.

“ hatuwezi kujiingiza kwenye kilimo cha kahawa kwani tunaona wazee wetu jinsi ambavyo wanahangaika bila ya mafanikio yoyote tofauti na miaka ya nyuma” alisema Kibona

Kwa upande wake Meneja wa kituo cha Taasisi ya Utafiti wa kahawa nchini (TaCRi) kilichopo Mbimba wilayani hapa Isaac Mushi alikiri zao la kahawa kukabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi ambapo kuna kiangazi cha muda mrefu ambacho kinaathiri zao hilo.

Sambamba na hilo ili kuongeza uzalishaji na kukabiliana na magonjwa sumbufu Mushi alishauri wakulima kupanda miche mipya iliyofanyiwa utafiti na taasisi yake inayokinzana na magonjwa hayo sumbufu.

Aidha aliongeza kuwa hivi sasa taasisi hiyo inaendelea na utafiti ili kupata miche ambayo inastahimili ukame ili kunusuru na kufanya uzalishaji uongezeke .

Mkulima toka Isansa ambaye pia ni diwani wa kata hiyo Emir Mzumbwe alisema wanakosa mvua za vuri zinazotarajiwa kuanza Septemba hadi Novemba ambazo zingesaidia kuchavusha,  lakini kukosekana kwa mvua hizo ni chanzo cha zao kuporomoka na kutokuwa na tija.

Alisema iwapo halmashauri haitachukua hatua za makusudi kujenga mabwawa ya umwagiliaji zao linakufa na itabaki historia, alitoa mfano katika bajeti ijayo kuwa fedha iliyotengwa kuendeleza zao hilo ni Sh. 75milioni na mwaka jana zilitengwa Sh. 60milioni hali ambayo inatishia usalama wa zao.

Kwa upande wake kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Elisey Ngoi alikiri kuwa uzalishaji wa kahawa unayumba kulingana na msimu kuwa iwapo mvua za vuri zikinyesha vizuri uzalisaji huongezeka na zikiwa mbaya unashuka, alitowa mfano kuwa katika msimu 2015/2016 uzalishaji ulikuwa tani 15260, lakini msimu wa 2016/2017 ulishuka hadi tani 8558 na msimu 2014/2015 tani 7665.

‘ tunawahamasisha wananchi watunze vyanzo vya maji ili kulinda uzalishaji na kuondokana na kutegemea mvua kwa asilimia kubwa” alisema Ngoi.

Aidha aliongeza kuwa halmashauri inatambua umuhimu wa mabwawa ya umwagiliaji, lakini alisema ili kufanikisha hilo panahitajika utafiti wa kutosha na fedha nyingi, hata hivyo alisema tayari mabwawa mawili yamechimbwa katika vijiji vya Msia na Hamwelo na kuwa wataendelea kuchimba mabwawa zaidi kadiri watakavyokuwa wakipata fedha.

Zaidi ya asilimia 70 ya mapato ya ndani ya halmashauri hiyo  ambayo ni zaidi ya Sh. 3.5 bilioni yanatokana na pato la zao la kahawa, lakini fedha inayotengwa ili kuboresha zao hilo ya Sh. 75milioni ni kidogo.
Mwisho.


No comments:

Post a Comment