Social Icons

Monday, 20 March 2017

Daraja la TASAF Mbozi Latelekezwa



Na: Stephano Simbeye, Mbozi

Wananchi wa vitongoji vya Mantengu A na B pamoja na Mwenge wilayani Mbozi mkoani Songwe wameiomba serikali kukamilisha ujenzi wa daraja linalounganisha vitongoji hivyo kwenda makao makuu ya wilaya ambako zinapatikana huduma za jamii baada ya daraja hilo kutelekezwa likiwa ,inajengwa kupitia mpango wa TASAF II iliyotoa zaidi Sh. 26 milioni.

Wakizungumza jana na gazeti hili wakazi hao walisema serikali kupitia halmashauri ya Mbozi imewatenga kwa kutowapelekea huduma muhimu za jamii ikiwa ni pamoja na barabara na vivuko na kufanya wananchi hao hususani wanawake wajawazito na wanafunzi kushindwa kuvuka hasa kipindi cha mvua ambapo maisha yao yanakuwa hatarini. Habari zaidi ingia songwemedia.

Vumilia Kabongo mkazi wa kitongoji cha Mantengu A, alisema wanapata adha kubwa hasa wanapovuka kwenda kuzika upande wa pili yalipo makaburi na kulazimika kuzunguka njia ndefu zaidi ya kilometa 20 badala ya kilometa mbili (2) huku kikwazo ikiwa ni ukosefu wa daraja.

Steven Simwembe alisema walitangaziwa kuwa zimetengwa Sh. 26 milioni kwa ajili ya kujenga daraja hilo ambalo tangu watangaziwe na kazi ya ujenzi kuanza na ghafra ukatelekezwa na sasa imepita miaka saba na kupelekea adha kubwa ya mawasiliano katika maeneo hayo mawili kwenda kupata huduma makao makuu ya wilaya ambako kuna hospitali ya wilaya, soko na shule ya msingi na sekondari Vwawa.

Mmoja wa wanafunzi Daniel Kalinga kutoka kitongoji cha Mantengu B alisema wanalazimika kukosa masomo katika kipindi cha mvua kutokana na mto kujaa, hivyo aliiomba serikali kukamilisha daraja hilo haraka ili kuondoa usumbufu wanaoupata.

Florida Chaming’ombe  mkazi wa matengu A alisema wakati anaelekea hospitali ya wilaya kwa ajili ya kujifungua alijikuta anajifungulia njiani kufuatia kupita njia ndefu kwa kuhofia kufa, kuepuka kupita kwenye daraja hilo ambalo wakati huu wa masika mto umejaa.

Mwenyekiti wa kitongoji cha Mwenge Abraham Kalonge alikiri kuwepo kero ya mawasiliano katika eneo hilo na kuwa wamekuwa wakilipigania suala hilo katika vikao mbalimbali vya mamlaka ya mji wa Vwawa pasipo mafanikio na kuiomba serikali kuliangalia tatizo hilo kwa jicho la tatu ili kunusuru maisha ya watu.

Kwa upande wake Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Erisey Ngoi licha ya kukiri daraja hilo kutengewa kiasi hicho cha fedha huko nyuma, alisema fedha hizo hazikutosha kukamilisha na kwamba halmashauri imeandaa mpango mkakati ili kumalizia daraja hilo ambalo kazi iliyosalia ni kumimina zege la juu.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment