Social Icons

Wednesday, 15 March 2017

Mazao yaaua Msangano

Stephano Simbeye, Mwananchi
ssimbeye@mwananchi.co.tz

MOMBA: Wakulima wa kata ya Msangano katika wilaya ya Momba mkoani Songwe, wameingiwa na hofu ya kukumbwa na njaa msimu ujao, baada ya mazao ya mpunga na mahindi waliolima mwezi Desemba kukauka kufuatia kukosekana mvua za vuri za mwezi January na Februari mwaka huu.
 
Baadhi ya wakulima waliohojiwa na mwandishi wa habari hizi walisema mvua za vuri zilianza kunyesha mwezi Desemba badala ya Novemba kama ilivyozoeleka ambapo walianza kulima na kupanda mahindi na kusia mbegu za mpunga kwenye vitaru, hata hivyo baada ya kuota mvua haikunyesha mwezi mzima wa Januari hadi wiki ya tatu ya mwezi Februari ambapo tayari mazao yalikuwa yamekauka.
 
Mkazi wa kijiji cha Ntinga Emanuel Sinkamba alisema hali ya ukame imewafanya washindwe kuelewa hatima ya maisha yao kutokana na kuwa fedha waliyokuwa nayo waliitumia kujiandaa na kilimo hicho ambapo sasa mazao yamekauka na kutokana na hali ngumu wanashindwa kuzitumia mvua zinazonyesha sasa kupanda mazao mengine ya muda mfupi.
 
"Tunaomba tusaidiwe mbegu za mtama za muda mfupi ili tutumie mvua zinazoendelea sasa kupanda mazao ya muda mfupi" alisema Sinkamba.
 
Mwenyekiti wa kijiji cha Msangano Simon Sichalwe alisema kutokana na ukame ambao umeathiri mazao yao hali ya chakula kijijini hapo itakuwa ngumu msimu ujao kutokana na kuwa hawatavuna kama inavyokuwa miaka mingine.
 
Alisema mazao wanayolima katika eneo hilo ni pamoja na Mpunga na mahindi ambayo huanza kupandwa mwezi Novemba kila mwaka na kuwa inapofika mwezi Machi na April yanakuwa yamekomaa, lakini hali ni tofauti mwaka huu ambapo mvua zilichelewa kuanza na pia zilisimama kwa muda mrefu kati ya Januari na Februari.
 
Kaimu ofisa kilimo wilayani Momba aliyejitambulisha kwa jina moja la Kiondo akizungumza kwa njia ya simu alikiri kuwapo ukame katika vijiji vitatu katika kata ya Msangano, ambavyo ni Msangano, Ntinga na Ipata na kijiji kimoja cha Nkara katika kata Chitete hata hivyo alisema wanawahamasisha wakulima kuanza kupanda mazao yanayostahimili ukame na yanayokomaa kwa muda mfupi kama mtama na mihogo.
 
Kuhusu takwimu halisi za hasara na uzalishaji uliotokea, alisema hawezi kuzitoa kwa vile yuko nje ya ofisi kikazi hata hivyo aliongeza kuwa ukame huo ungeathiri pia kata nzima ya Chitete lakini kutokana na kuwepo mradi wa umwagiliaji wa Naming’ongo umesaidia wakazi wengi wa kata ya Chitete kulima mazao yao kwa kumwagilia.
 
Jitihada za kumpata Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya wilaya Momba Adriano Jungu ili kuzungumzia madhara yaliyosababishwa na ukame huo, na jitihada za halmashauri hiyo kusaidia upatikanaji wa mbegu za mtama na mhogo hazikuzaa matunda baada ya kutopokea simu yake ya mkononi kwa muda mrefu na hata alipoandikiwa ujume mfupi wa maneno (SMS) hakujibu lolote.
 
Aidha eneo hilo ndilo linalotegemewa kwa uzalishaji wa mpunga ambao hulisha maeneo ya Tunduma, Mbalizi (Mbeya vijijini) na maeneo ya Mlowo na Vwawa katika wilaya ya Mbozi, hivyo yatakabiliwa na upungufu wa mpunga.
Mwisho.
 
 

No comments:

Post a Comment