Social Icons

Monday, 20 March 2017

POMBE ZA VIROBA MBOZI ZAPEWA JINA JIPYA LA SUB UFA, SAMAKI MKAVU NA MAZIWA





Na: Stephano Simbeye, Mbozi

Juhudi za serikali za kukomesha pombe kali za viroba huenda zikakwama baada ya baadhi ya wafanyabiashara wilayani Mbozi mkoa wa Songwe kubuni njia mpya ya kuuza vinywaji hivyo vilivyopigwa marufu kwa kuvibatiza majina mapya ya Sub Ufa, Samaki mkavu au maziwa.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi kwa siku tatu wilayani hapa katika maeneo mbalimbali yanayouza vinywaji hivyo, imeshuhudiwa kuwa wahudumu wa maeneo hayo wanawafahamu wateja wao ambao wakifika hutamka majina hayo na kisha kupewa huduma kimya kimya.

Neema Mwampashe mmoja wa wamiliki hao aliiomba serikali kuwaongezea muda ili waviondoe viroba hivyo kwa kuwa biashara zao wanaendesha kwa fedha za mkopo ambapo wamekuwa wakirejesha kila mwezi baada ya mauzo na wao wanategemea zaidi biashara hiyo ambayo inawapatia faida kubwa.

Mmoja wa wateja waliokutwa wakijipatia kinywaji hicho Daniel Simwinga mkazi wa Vwawa alisema kuviondoa viroba vitawapa wakati mgumu kutokana na kuwa vimekuwa vikiuzwa kwa bei nafuu ambayo wao wenye kipato kidogo wanamudu gharama za kuvinunua.

Alisema wanaiomba serikali kutafuta njia mbadala ya kuviweka viroba hivyo kwenye chupa na kuuza kwa bei nafuu ili waweze kumudu kuvinunua kwa kuwa pombe hiyo si haramu bali kinachokatazwa ni karatasi.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya wafanyabiashara wilaya ya Mbozi Yohana Mwajeka (JEKAS) alikiri kuwa wafanyabiashara wamebadilisha majina ya vinywaji hivyo na kusema kuwa ili serikali ifanikiwe kudhibiti biashara hiyo itumie busara kwa kuwajali wafanyabiashara kwa kuongezea muda wa kuviondoa viroba sokoni.

Alisema ilitakiwa viroba hivyo virudishwe viwandani ili vikawekwe kwenye chupa na kurudishwa sokoni badala ya kuvikataza ili hali wengi walikuwa na shehena kubwa ambayo ililipiwa na kodi stahiki za serikali vikiwa tayari vimewekwa nembo ya ubora toka shirika la viwango nchini (TBS).

Aidha mwanzoni mwa mwaka huu serikali kupitia kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kasim Majaliwa aliagiza kwamba ifikapo Marchi mosi mwaka huu vinywaji hivyo viwe vimeondoka sokoni ili kunusuru vijana wengi ambao wamekuwa wakivinunua kwa bei ya chini na kunywa nyakati zote pasipo kufanya kazi, tangu tarehe  hiyo mamlaka husika zimekuwa zikifanya msako na kukamata pale wanapopata bidhaa hiyo inauzwa.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment