Social Icons

Tuesday, 7 March 2017

Mbunge Asoma Taarifa ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Mfuko wa Jimbo



Stephano Simbeye, mwananchi
MBOZI: Mbunge wa jimbo la Mbozi mkoani Songwe, Pascal Haonga (Chadema) amewasomea wapiga kura wake taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za mfuko wa jimbo zaidi ya Sh.76milioni alizopata kwa awamu mbili tangu achaguliwe kushika wadhifa huo mwaka 2015 kitendo ambacho hakijawahi kufanywa na watangulizi wake.

Hatua hiyo aliifanya jana katika hafla ya kukabidhi kisima alichokichimba katika mji wa Mlowo wilayani hapa ambapo alisema fedha za mfuko wa Jimbo si mali ya Mbunge bali zinatokana na kodi zao, hivyo ni lazima wapate taarifa ya jinsi zinavyotumika na kuwa serikali inatowa fedha hizo ili kuchochea na kuchangia nguvukazi katika miradi ya wananchi.

Haonga alisema mwaka jana mfuko huo ulipokea Sh. 33milioni ambazo alizielekeza katika miradi ya kuweka vifaa vya umeme jua katika zahanati pamoja na kukamilisha vyumba vya madarasa katika vijiji 17, ili kuunga mkono nguvu za wananchi ambao walijenga kufikia hatua ya mtambaa panya pamoja, kujenga daraja la kuunganisha vijiji vya Shasya na Halungu na kununua tenki la kuhifadhia maji katika kijiji cha Igamba.

Akizungumzia fedha nyingine ya mfuko wa jimbo ambayo imepokelewa hivi karibuni kiasi cha Sh.43 milioni alisema fedha hizo zitatumika kukamilisha vyumba 21 vya madarasa na ofisi 3 za walimu, nyumba 2 za walimu, kukamilisha majengo 5 ya zahanati na vyoo matundu 18 na kununua vifaa vya umeme jua katika zahanati ya Iwalanje.

Akizungumzia kisima cha maji alichokizindua katika mji mdogo wa Mlowo Haonga alisema kimegharimu zaidi ya Sh. 11milioni fedha ambazo zaidi ya sh. 10.4 milioni zimetoka mfukoni mwake, na Sh. 660000 zimetolewa na serikali ya kijiji.

Mmoja ya wakazi wa Mlowo Onesmo Kapungu alisema kitendo cha Mbunge huyo kuwasomea taarifa ya mapato na matumizi wananchi wake kimeonesha njia kwa watendaji wengine kufanya hivyo na kuwa hakuna mbunge aliyewahi kufanya hivyo.

Naye Rahel Lyanda alisema Mbunge ameonesha njia kwa wengine kufuatia uamuzi wake wa kuwafafanulia na kuwajulisha juu ya fedha zao za mfuko wa jimbo ambazo hawajawahi kufahamu kama zinaingia ngapi na zinatumikaje.

Mganga mfawidhi wa Zahanati ya Mlowo Semeni Mswima ambako kilizinduliwa kisima kwa ajili ya kuwapatia huduma ya maji wagonjwa na wakazi wa jirani na eneo hilo, alisema maji hayo yatasaidia kupunguza kero ya maji wanayopata kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo kunywa.

Aidha mganga huyo alisema katika zahanati hiyo wengi wanaofika kupata matibabu wanasumbuliwa na magonjwa yanayotokana na kunywa maji yasiyosafi na salama ya kuhara, homa ya matumbo na kuhara damu.
Mwisho  

No comments:

Post a Comment