Social Icons

Thursday, 30 March 2017

Vijana Waishutumu Halmashauri ya Mbozi kwa Urasimu

Stephano Simbeye, Mbozi
 
Vijana wameilalamikia halmashauri ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, kuwa na milolongo mirefu ya utoaji mikopo kwa vijana na wanawake hali inayowakatisha tamaa na kusababisha washindwe kujikwamua kiuchumi.
 
Malalamiko hayo yalitolewa jana mjini Vwawa wakati wa uzinduzi wa mradi wa ushirikishwaji vijana katika sekta ya kilimo na ufugaji utakaowanufaisha zaidi ya vijana 2000 wilayani hapa katika kipindi cha miaka mitano tangu 2016 hadi 2021 unaoendeshwa na shirika la Heifer International ambapo watapatiwa stadi za mafunzo ya ujasiriamali kwa vitendo.
 
Jakob Mkisi ni mmoja wa vijana hao alisema kundi la vijana bado ni tegemezi lisilomiliki rasimali yoyote, huku likabiliwa na ukosefu wa ajira wakati wengi wao wakiwa ndiyo kwanza wametoka masomoni kuwa kundi hili linahitaji uwezeshi na uangalizi wa aina yake ili kuweza kujikomboa kiuchumi kwa kujiajiri ili nao waweze kutoa mchango kwa pato la taifa.
 
Alisema kutokana na uchanga wao wanakosa kujiamini katika kusimamia mambo mbalimbali ambayo yatawasaidia kuiandaa kesho yao kwa kufanya kazi leo kutokana na wengi kutaka utajiri wa haraka, pia changamoto ya kuwapo na milolongo mirefu ya upatikanaji wa huduma inawakatisha tamaa na ukosefu wa njia sahihi ya upashanaji habari wanajikuta wanaingia katika makundi yasiyo sahihi.
 
Peter Mwansite ni kiongozi wa kundi la vijana la Focus Forward akizungumzia tatizo la ajira kwa vijana alisema ni vema wazazi wakaona umuhimu wa kuwapatia rasilimali kidogo ambazo zitawasaidia kuanzishia miradi ya kujiajiri huku mamlaka husika zikisaidia kuwaondolea urasimu wa upatikanaji mikopo na kuwapatia stadi za mafunzo stahiki.
 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Elick Ambakisye alisema halmashauri yake imeupokea mradi huo kwa mikono miwili na kuwa itatoa ushirikiano wa dhati kuhakikisha malengo yake yanatimia kwa kufanya kazi bega kwa bega na Shirika na makundi mbalimbali ya vijana ili kuwakwamua na tatizo la ukosefu wa ajira.
 
Aidha alisema zipo changamoto nyingi zinazojitokeza katika utoaji wa mikopo ya vijana na wanawake, ikiwemo kushindwa kurejesha mikopo na kuwa hata hivyo halmashauri imejipanga upya kuona hilo halijitokezi.
 
Naye Mkuu wa mkoa wa Songwe Chiku Galawa akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi wa mradi aliziagiza halmashauri mkoani humu kutenga maeneo ya kutosha kwa ajili ya vijana ambapo alisema utengaji wa maeneo uende sambamba na kuhakikisha asilimia 10 ya makusanyo ya mapato yake zinakwenda kwa makundi ya vijana na wanawake.
 
Aidha Galawa alisema fedha hizo hazitolewi kwa hiari bali ni lazima na ni haki ya makundi husika hivyo halmashauri ambayo itashindwa kufanya  kutoa fedha hizo mkurugenzi atawajibishwa.
 
Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Shirika la Heifer International Damas Damiani alisema mradi huo unalenga kuwajengea stadi za ujasiliamali vijana wenye umri kuanzia miaka 18 hadi 24 kundi ambalo limekuwa halijihusishi na kilimo na ufugaji ili nalo liweze kuona kuwa sekta hiyo inaweza kuwapatia ajira na kuwaongezea kipato.
 
Alisema vijana hao watapangwa katika makundi mbalimbali kulingana kazi watakazochagua wenyewe kuzifanya na kisha baada ya hapo watakuwa wakipatiwa mafunzo na stadi mbalimbali za uzalishaji mali
Mwisho.

No comments:

Post a Comment