Social Icons

Wednesday, 1 March 2017

Wafanyabiashara wameiomba serikali kuufungua mji wa Vwawa



Na Stephano Simbeye, Mbozi

Wafanyabiashara katika mji wa Vwawa wilayani Mbozi mkoani Songwe, wameiomba serikali kuufungua mji huo na maeneo mengine kwa kuboresha miundombini ya barabara ili kurahisisha mawasiliano katika usafirishaji na uchukuzi ili kusaidia kuvutia wawekezaji. 

Kilio hicho kiliwasilishwa jana katika mkutano uliofanyika mjini hapa kwa Mbunge wa jimbo la Vwawa Japheti Hasunga (CCM)walipokuwa wakiwasilisha kero zinazowakabili na Greenwell 

Nsyukwe (Jack Msafwa) ambaye alisema mji huo umekuwa kisiwa licha ya kuwa ni makao makuu ya mkoa kutokana na kukosa mawasiliano ya uhakika na maeneo mengine jirani hali ambayo inasababisha ufanyaji wa biashara kuwa mgumu.

"Mheshimiwa Mbunge hebu tusaidie kufungua barabara za kuingia katika mji wetu ambapo zilizopo ni chafu zisizopitika wakati wote na kufanya kuwa kero kwetu inayotufanya tushindwe kufanya biashara" alisema Greenwell.

Alitaja baadhi ya njia ambazo endapo zikiboreshwa zitarahisisha mawasiliano kuwa ni pamoja na barabara ya Ilembo  Mahenje hadi Kimondo, Hasamba Nyimbili hadi Ileje, Hasamba Izyila hadi Mbeya vijijini na Igamba Mbozi Club ambazo ni muhimu kwa uchumi wa mji huo.

Nivard Lwila alisema mji huo umezorota kibiashara kutokana na kuwa hauna wageni wanaoingia kutokana na kutokuwa na barabara zinazopitika wakati wote huku serikali ikiwa haijaonesha mikakati yoyote ya kuboresha barabara hizo.

“ tumejiandaa kuwekeza ili tuzitumie fursa za kuanza kwa mkoa mpya lakini bado kikwazo ni miundombinu ambayo ni muhimu kwa ajili ya usalama vyombo vya uchukuzi na mji wowote ule unahitaji mawasiliano ili watu wake kujiletea maendeleo lakini hapa tunakosa huduma hiyo” alisema Lwila.

Naye mfanyabiashara Edward Mahenge (Ndisana) alieleza kusikitishwa kwake jinsi sheria ya zimamoto inavyotekelezwa kwa kuwalazimisha kutoa fedha za ada pasipo kuelimishwa, badala yake watendaji wake wamekuwa wakipita kwenye biashara zao wakiwa na askari Polisi huku wakiacha vitisho ukuki.

“ tunaona huu ni ubabe usio na msingi wanafika kwenye biashara kudai fedha wakati hata huduma yenyewe ya zimamoto hatuioni kwanini kusiwekwa utaratibu wa kutekeleza mambo kama haya ili mtu aelewe anatoa fedha kwa ajili gani”alisema Ndisana.

Akijibu hoja za wafanyabiashara hao Mbunge Hasunga alikiri kutambua kero hiyo, lakini alisema neema ya kuanzishwa kwa mkoa wa Songwe itasaidia kuwepo kwa wakala wa barabara (TANROAD) ambao   inapata fedha nyingi za matengenezo ya barabara ukilinganisha na halmashauri ambao zitasaidia kutengeneza barabara hizo ili zipitike wakati wote.

Alisema mipango ya mkoa ni kufungua njia tatu muhimu ambazo ni pamoja na barabara ya Mbozi Club kupitia Igamba hadi Mkwajuni wilayani Songwe, barabara ya Vwawa kupitia Nyimbili Hezya hadi Ileje na barabara ya Ihanda Chindi hadi Chitete wilayani Momba, na kuwa iwapo barabara hizo zitafunguka zitasaidia kurahisisha mawasiliano mkoani hapa na pia kuufungua mji wa Vwawa.

Aidha Hasunga aliwataka wafanyabiashara hao kuanza kuchangamkia fursa za ujio wa wageni wataalamu mbalimbali wamaoletwa kuja kufanya kazi mkoani hapa, kwa kujenga nyumba nzuri za kupangisha ili wajiongezee kipato na fursa nyingine ni ya kuwa wageni hao watahitaji vyakula na mahitaji mengine ya kibinadamu.

 Naye Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Mbozi Elisey Ngoi alisema katika bajeti ya halmashauri hiyo mwaka ujao wa 2016/2017 imeweka vipaumbele vitatu ambavyo ni kujenga barabara na madaraja, kukamilisha vyumba vya madarasa na zahanati vilivyojengwa na wananchi na kulipa madeni ya wazabuni wake, hali itakayofanya mji huo kuwa na barabara zinazopitika wakati wote.

Aidha mji wa Vwawa ambao ni makao makuu ya mkoa wa Songwe unakabiliwa pia na changamoto ya barabara za mitaa zenye hadhi ya makao makuu ya mkoa
Mwisho.

No comments:

Post a Comment