Social Icons

Thursday, 6 April 2017

CCM Yamuondolea Dhamana Mwenyekiti wa Halmashauri

Stephano Simbeye, Mwananchi
VWAWA: Chama cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbozi mkoani Songwe kimemuondolea udhamini Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Erick Ambakisye kwa madai ya kushindwa kuisimamia halmashauri, na kusababisha upotevu wa fedha za umma na upatikanaji wa hati zenye mashaka kwa miaka minne mfululizo.

Hayo yalisemwa jana na Kaimu Katibu wa chama wilayani hapa George Silindu kuwa kamati ya siasa ya chama hicho iliyokutana April mosi mwaka huu kiliazimia kuondoa dhamana yake kufuatia tuhuma mbalimbali zinazomkabili ambazo zimesababisha chama hicho kukosa imani kwa wananchi.

Alizitaja baadhi ya sababu hizo kuwa ni upotevu wa Sh. 410milioni ambazo chama hakijui mstakabali wake kwa muda mrefu, kupatikana na kwa hati zenye mashaka kufuatia ukaguzi unaofanywa na Mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali kwa miaka minne mfululizo na kushindwa kusimamia maamuzi ya kuweka makao makuu ya kata ya wasa kwa kutofautiana na chama.

Mwenyekiti wa chama hicho wilaya ya Mbozi Aloyce Mdalavuma alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya kuona kiongozi huyo hakidhi matakwa ya chama, ambapo makosa yake yamesababisha malalamiko mengi toka kwa wananchi kufuatia mwenendo mbovu wa halmashauri ya Mbozi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa halmashauri ya Mbozi Erick Ambakisye akizungumzia suala hilo alisema hajapata rasmi barua ingawa amekuwa akisikia yakizungumzwa mtaani, hata hivyo alisema kinachoendelea kinatokana na mambo ya kisiasa na vita dhidi ya nafasi ya uenyekiti na uchaguzi mkuu wa 2020.

Alisema vita hiyo ilianza muda mrefu ambapo yamekuwepo majaribio mara sita ya kutaka kumuondoa kwa njia ya kushawishi madiwani kupiga kura ya kutokuwa na imani naye, majaribio ambayo hayakuzaa matunda.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi Lusajo Mwalukasa amekiri kupokea barua kutoka kwenye chma cha mapinduzi ikimuagiza kumjulisha mwenyekiti huyo kuwa ameondolewa udhamini, hata hivyo alisema taratibu za kumuondoa mwenyekiti zimekiukwa kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazoendesha halmashauri vifungu vya 82 (1) (a hadi E) ambavyo vinaenda sambamba na tangazo la serikali namba 262 la 1998.

Aliongeza kuwa taratibu za kumuondoa mwenyekiti wa halmashauri ambaye ni kiongozi wa baraza la madiwani wa vyama vyote ambao ndiyo waliomchagua zinataka ipatikane orodha 2/3 ya wajumbe wa baraza la madiwani na kasha kuweka sababu za kutaka kumuondoa, ambapo mkurugenzi atamuandikia mwenyekiti ambaye atahitajika kuzijibu kwa muda wa siku tano kwa maandishi ikiwa ni utetezi wake.
Mwisho
 

No comments:

Post a Comment