Social Icons

Thursday, 6 April 2017

Viroba vyateketezwa



Stephano Simbeye, Mbozi

Jeshi la Polisi wilayani Mbozi mkoani Songwe, jana limeteketeza pombe za viroba zilizokamatwa kwenye operasheni iliyofanywa hivi karibuni zenye thamani ya zaidi ya Sh. 2.5 milioni, baada ya washitakiwa waliokamatwa wakiviuza, kesi zao kutolewa hukumu na mahakama ya mwanzo Vwawa mjini.

Akizungumza mara baada ya zoezi hilo Mkuu wa operesheni wa jeshi hilo Mkaguzi wa Polisi Simon Mwavea amesema hatua hiyo imefikiwa baada ya watuhumiwa kufikishwa mahakamani na kutolewa hukumu ambapo wahusika  wamepewa adhabu mbalimbali ikiwemo kifungo na wengine kulipa faini.

Alisema operasheni ya kukamata viroba katika mji wa Vwawa imesaidia kupunguza matukio ya uharifu baada ya vijana waliokuwa wanalewa asubuhi, kuacha kufanya hivyo na kuanza kufanyakazi ambapo wengi wamejiajiri kwenye bodaboda, wengine katika vibarua mbalimbali ikiwemo kazi za shambani.

Mwavea ameonya wale wote ambao bado wanaendelea kuuza viroba kwa kuvipa majina tofauti kuwa jeshi hilo linaendelea na operesheni na watakaokutwa navyo hatua kari zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kunyang’anywa na kufikishwa mahakamani, pia amewataka viongozi wa vijiji, vitongoji na mitaa kuacha kuwalinda wauza viroba.

Mmoja wa wananchi aliyeshuhudia zoezi la kuteketeza viroba hivyo Manuel Kaminyoge amesema kutokana na urahisi wa upatikanaji vinywaji hivyo vilisababisha ulevi ambao ulikuwa chanzo cha matukio ya uharifu na pia unarudisha nyuma uchumi wa vijana na taifa kwa ujumla.

aidha mara baada ya viroba kupigwa marufuku na serikali wauzaji wamebuni mbinu mpya ya kuuza kwa kuviita majina mapya ya Sub ufa, maziwa fresh, biscuti na mengine mengi
Mwisho


No comments:

Post a Comment