Stephano Simbeye, MBOZI
Wakazi wa Vijiji vya Wasa na Malolo katika kata ya Wasa wilayani Mbozi mkoani Songwe
wamevunja ushirikiano wa kijamii na
wenzao wa vijiji vya Isalalo na Izyaniche kutokana na ugomvi wa kugombea
makao makuu ya kata hiyo, na kumzuia ofisa mtendaji kata na kijiji cha Wasa,
mpaka serikali itakaporejesha ofisi za kata katika eneo zilipokuwepo awali.
Sakata hilo ambalo limedumu takribani miaka miwili sasa linadaiwa
ni kufuatia uamuzi wa diwani kata hiyo kuamua kuhamisha ofisi za kata hiyo toka
kijiji cha Wasa na kuzihamishia kijiji cha Isalalo kwa kigezo cha kuwa ni
katikati ya vijiji vyote vinne vinavyounda kata hiyo jambo ambalo liliibua
mgogoro baada ya wananchi wa vijiji viwili vya Wasa na Malolo kupinga wakidai
kuwa vijiji vyao vina wakazi wengi.
Joseph Sinkonde mkazi wa kijiji cha Wasa alisema wameamua kumzuia mtendaji wa kijiji
kufanyakazi kijijini hapo hadi pale ambapo serikali itakaporejesha ofisi za
kata katika kijiji cha Wasa zilipokuwa tangu kuanzishwa mwaka 2015.
“ kutokana na kitendo hicho cha kuhamisha makao makuu ya
kata toka Wasa kwenda Isalalo hatuko tayari kushirikiana na watendaji wala
serikali tutabaki na shida zetu mpaka kitakapoeleweka” alisema Sinkonde.
Mawazo Andondile
alisema suala la mgogoro wa kugombea makao makuu ya kata limeathiri pia
mahusiano ya kijamii, watu hawauziani wala kununuliana alitoa mfano kuwa kila tarehe 8 ya mwezi katika kijiji cha
Isalalo kunafanyika gurio, lakini watu wa Wasa na Malolo hawashiriki, na hata
katika shughuli za misiba wameacha kushirikiana wakihofia kudhuriana kutokana
na mgogoro huo.
Alisema mgogoro huo umeenda mbali zaidi baada ya wanafunzi
84 waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza katika shule ya sekondari Isalalo
mwaka huu wamehamishwa shule hiyo na
wazazi wao, na kuwahamishia shule jirani ya Msia kutokana na hofu ya mzozo huu kwa usalama wao.
Mmoja wa wazazi wa wanafunzi waliohamishwa shule hiyo
Wiliadi Mnkondya alisema uamuzi wa kumhamisha mwanaye ni kutokana na kukosekana
kwa amani kufuatia hofu ya usalama wa
mtoto wake na kudai kuwa hata hivyo shule ya Msia iko karibu ukilinganisha na
Isalalo.
Mkazi wa kijiji cha Isalalo Joseph Damiani alisema uamuzi wa
kuweka makao makuu ya kata kijiji cha Isalalo ulikuwa sahihi ili kuwasogezea
huduma wakazi wa vijiji viwili kati ya
vinne vinavyounda kata hiyo ambavyo viko
mbali na huduma za kiserikali hali iliyosababisha kujiona kama
wametengwa na serikali yao.
Alisema suala hilo limepoteza amani ambapo wenzao wa vijiji
viwili vya Wasa yenye wakazi 4800, Malolo wakazi 2700 na Isalalo wapo wakazi 2600
na Izyaniche wapo wakazi 1000 na kuwa madai yanayotolewa na wenzao wa vijiji
hivyo ni ya kibinafsi zaidi ambayo wanaona yanawatenga licha ya kuwa wote ni
jamii moja.
Kwa upande wake
Diwani wa kata hiyo ambaye pia anatokea kijiji cha Isalalo Ezekiel Mwashambwa akizungumzia sakata hilo
alisema sababu za kuhamisha makao makuu
ya kata ni kutokana na kuwa baadhi ya vijiji vilikuwa mbali na ofisi za kata
ndipo walipopendekeza kwa halmashauri ya wilaya kuhamisha ofisi za kata ili
ziwe katikati ya vijiji vyote vinne, ndipo kamati ya madiwani ya uchumi na
mazingira ilipofika kujiridhisha na kupendekeza kwenye baraza kamili la
madiwani ambalo lilidhia kuhamishwa ofisi hizo.
Alisema uamuzi wa kuhamisha makao makuu ya kata ulipokelewa
kwa mtazamo hasi na wakazi wa vijiji vingine viwili vya Wasa na Malolo hali
iliyosababisha kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi wilaya Mbozi kufika
katani hapo ndipo ilikutana na mabango yaliyodai kuwa kata haihamishiki na
kutaka kumpiga diwani huyo hali iliyosababisha kukimbizwa na gari la chama
lenye namba za usajili T. 595 BEW na kisha
kikao hicho kuvurugika.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Mbozi Elisey Ngoi akizungumza kwa njia ya simu na mwandishi
wa habari hizi jana alikiri kuwapo na
mgogoro wa kugombea makao makuu ya kata katika kata hiyo na kudai kuwa suala
hilo linafanyiwa kazi kwa kutumia busara
kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Songwe.
“ tumeona suala hili tulitatue kwa kutumia busara zaidi
badala ya kulichukulia kama ugomvi na
njia nyingine kwani tunaona zitaharibu zaidi na kuendelea kuhatarisha amani
katika maeneo hayo”alisema Ngoi.
Hata hivyo alikanusha kuwa wanafunzi 84 wa shule ya sekondari Isalalo waliohamia
Msia ni kutokana na mtafaruku uliopo, bali alisema ni kutokana na kuwa Msia
sekondari ipo jirani zaidi na makazi ya watoto hao ukilinganisha na Isalalo na
kuwa katika kuthibitisha hili wazazi wa watoto hao kwa hiari yao walishiriki
kukamilisha vyumba vya madarasa kwa nguvu yao ili watoto waanze kusoma.
Mwisho
No comments:
Post a Comment