Social Icons

Thursday, 11 May 2017

MLOWO WAKUBALI MAKAZI YAO KUPANGWA UPYA



Stephano Simbeye, MBOZI

Mlowo: Wakazi wa kitongoji cha Mtakuja katika mji wa Mlowo wilayani Mbozi mkoani Songwe, wameridhia makazi yao kupangwa upya ili kuwekwa miundombinu ya barabara na huduma nyingine za kijamii pasipo kulipwa fidia, ili makazi yao yathaminishwe na kupatiwa hati miliki ya ardhi huku wakitahadharisha wanasiasa kutoingilia zoezi hilo.

Makubaliano hayo yalifikiwa  jana wakati wa mkutano wa uhamasishaji kabla ya zoezi la kuanza kurasimisha na kupanga makazi yaliyojengwa kiholela, mpango unaofanywa na Mpango wa kurasimisha rasilimali na biashara Tanzania (MKURABITA) kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya ya Mbozi ambapo wakazi wa eneo hilo walilidhia licha ya kuitupia lawama serikali kufumbia macho wakati ujenzi holela ukiendelea.

Jeradi Mwashilindi mkazi wa eneo hilo alisema wanahamu kubwa ya kuona makazi yao yanaboreka na kuongezeka thamani kuliko ilivyo sasa ambapo makazi yao yanakataliwa na wageni wanaohitaji kupanga kutokana na  maeneo hayo kukosa barabara na kufanya yasifikike kirahisi.

"Mimi nilihamia hapa mwaka 1968 nikagawiwa kiwanja mwaka 1970 ambapo maeneo haya yalipimwa lakini yameendelea kuvamiwa taratibu huku mamlaka husika zikifumbia macho"alisema mzee Mwashilindi

Mkazi mwingine wa kitongoji hicho Mariam Mwinuka alitahadharisha zoezi hilo lisiingiliwe na wanasiasa kwa kuwa watawagawa watu kwa itikadi zao hali ambayo itazua migogoro itakayokwamisha mpango wa kurasimisha makazi yao.

Awali akihamasisha wananchi Ofisa mipango miji wa halmashauri ya Mbozi Vitus Mwanalinze alieleza hatua tatu kuelekea urasimishaji kuwa wameanza na hamasa, itafuatia kutambua makazi ambapo kila mmiliki atapaswa kuwepo ili kutoa taarifa sahihi baada ya hapo itaandaliwa michoro ya ramani (Deed plan) na kufuatiwa na urasimishaji wenyewe kazi hiyo itatumia muda wa siku 20.

Alisema katika kutekeleza kazi hizo hapatakuwa na fidia kwa makazi yatakayohitajika kubomolewa, bali wakazi wa kitongoji husika watakubaliana jinsi ya kufanya ili kufanikisha zoezi.

Mwanalinze alisema mji wa Mlowo mpaka sasa upimaji wa kawaida ulifanyika kwa asilimia 15 ambayo haiendani na kasi ya kukua kwake na kwamba halmashauri imekwama kupima eneo lililobaki kutokana na changamoto za kibajeti.

Naye ofisa Mtendaji wa kijiji cha Mlowo Judith Mtega alisema kijiji hicho chenye wakazi 21181 kwa mujibu wa sensa ya 2012,  lakini kinakabiliwa na ongezeko kubwa la watu na makazi unaotokana na watu kuingia ili kufanya biashara na kuwa chanzo cha ujenzi holela .

Meneja wa mpango wa kurasimisha rasilimali na biashara Tanzania (MKURABITA) Japhet Werema alisema katika kufanikisha kazi hiyo serikali metowa mtaji wa Sh. 17milioni ili kuanzia kazi hiyo ya kupima na kurasimisha ardhi ya wanyonge na kuwa wananchi kwa upande wao watachangia kidogo gharama hizo.

Alisema katika kutekeleza mpango huo wananchi walidhie wao wenyewe  kuachia baadhi ya maeneo ambamo barabara zitapita na huduma nyingine za kijamii ziweze kuwafikia kirahisi.
Mwisho

No comments:

Post a Comment