Social Icons

Tuesday, 9 May 2017

Momba Wafufua Kiwanda cha Chumvi

Na: Stephano Simbeye, Momba



MOMBA: Kiwanda cha Chumvi kilichopo katika kijiji cha Itumbula wilayani Momba mkoani Songwe kilichositisha uzalishaji miaka ya 80, kinatarajia kuanza uzalishaji mapema mwezi Julai mwaka huu, baada ya kufanyiwa ukarabati na halmashauri ya wilaya hiyo kufikia zaidi ya asilimia 90 na hivyo zaidi ya watu 3000 kuanza kunufaika.

Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Momba Adriano Jungu katika kikao cha Baraza kamili la Madiwani lililokutana mjini Chitete kuwa, kazi ya kusafisha kisima kinachotoa madini joto imekamilika na kuwa kazi inayoendelea ni kujenga mifereji ya maji ya mvua ili yasiingie kisimani na kuchafua chumvi na kufanya marekebisho mengine madogo madogo na kuwa zaidi ya Sh. 10 milioni zimetengwa kwa kazi hiyo.

Alisema iwapo kiwanda hicho kitaanza uzalishaji wananchi zaidi ya 3000 wakazi wa kijiji hicho wataanza kunufaika kwa kuongeza kipato pia halmashauri ya kijiji itaongeza mapato na halmashauri kwa ujumla itaongeza mapato yake ya ndani yatakayotokana na ushuru na mzunguko wa fedha utaongezeka kwa wafanyabiashara na kwamba uzalishaji wa chumvi kwa siku itakuwa kilogramu 500 au nusu tani.

“ Kiwanda hicho kilifungwa miaka mingi iliyopita kufuatia ubadhirifu wa viongozi wa ushirika waliokuwa wakisimamia, hata hivyo suala la uongozi limerekebishwa na kuwa halmashauri itakuwa karibu zaidi ili kuhakikisha changamoto hiyo haijitokezi tena” alisema Mkurugenzi Jungu

Akizungumzia suala hilo diwani wa kata ya Kapele Gaasto Simpassa alishauri wataalamu wanaofanyakazi za ukarabati eneo hilo kushirikiana na wenyeji ili wawasaidie kutoa baadhi ya ushauri ili kufanikisha kazi hiyo haraka.

Alisema wanayomatumaini na hamu kubwa kiwanda hicho kianze kazi ili waanze kunufaika na fursa zitakazoambatana na shughuli hiyo ikiwa ni pamoja na kuongeza kipato kufuatia ongezeko la watu na shughuli nyingi za kiuchumi na kijamiii.

Mkazi wa eneo hilo Yusta Sichela alisema mradi huo utaleta mabadiliko makubwa kijijini hapo kufuatia wageni wengi kwenda kununua chumvi na hivyo wamejiandaa kuanza kutumia fursa hiyo kuboresha masha yao kwa kuinua uchumi utakaotokana na huduma mbalimbali zitakazohitajika.

Alisema kiwanda hicho kilifungwa miaka ya 1980, changamoto zilizosababisha kiwanda kufungwa zitazamwe vizuri ili tatizo hilo lisijetokea tena na pia ameiomba serikali kuratibu kwa karibu shughuli za kiwanda hicho ambacho ni fursa ya kuongeza kipato kwa wakazi wa kijiji na wilaya kwa ujumla

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Methew Chikoti aliwataka wataalamu kuhakikisha wanasimamia kazi zilizosalia ili kukamilisha na uzalishaji wa chumvi uanze katika muda uliopangwa na kuwa wanatarajia kikao kijacho cha baraza la madiwani watapata taarifa ya kiwanda kuwa kimeanza kazi na si vinginevyo
Mwisho.

No comments:

Post a Comment