Social Icons

Friday, 12 January 2018

Wataalamu Shirikianeni na Wananchi Kuibua Vyanzo vya Maji



Stephano Simbeye, MBOZI: 

Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji Jumaa Hamidu Aweso amewataka wataalamu wa maji nchini kushirikisha wananchi katika kutafuta vyanzo vya maji na katika kutambua maeneo halisi yenye uhaba wa maji wakati wa kusambaza.

Kauli hiyo aliitoa jana katika kijiji cha Itaka kufuatia malalamiko ya mkazi wa kijiji cha Itewe Sikujua Mwankusye kuwa yameachwa maeneo halisi yenye uhaba wa maji badala yake yamepelekwa katika maeneo yasiyo na uhaba mkubwa na kuwaacha wananchi wakiendelea kutabika kupata maji huku wakiona wenzao wakineemeka wakati tayari wanapata huduma hiyo jirani na visima vya asili.

“ Mheshimiwa Naibu Waziri tunashangaa wataalamu kuweka vituo vya maji katika maeneo ambayo tayari kuna maji huku wakiacha kwenye mapungufu makubwa bila kituo chochote cha maji: alisema Mwankusye.

Mwenyekiti wa kijiji cha Itewe Efeso John alipoitwa kuelezea namna vituo vilivyopatikana alisema wataalamu wa maji walifika kijijini hapo na kasha kuanza kuonyesha maeneo yatakayowekwa vituo vya kuchotea maji na kwamba hawakushirikishwa ili kutambulisha kwenye uhaba wa maji.

Alisema baada ya kuona eneo moja ndani ya kijiji chao lenye uhitaji mkubwa wa maji halijawekwa kwenye mpango wa kupatiwa maji licha ya mradi kuwepo kijijini hapo walihoji lakini walijibiwa kwamba hawawezi kuyavusha maji barabara.

Mhandisi wa maji wilayani hapa Crispin Warioba alikanusha madai hayo na kueleza kwamba hatua zote serikali za vijiji na umoja wa watumia maji zilishirikishwa katika kutambua maeneo yote ambayo yaliwekwa kwenye mpango wa kuwekwa vituo vya kuchotea maji na kuwa madai yanayotolewa si ya kweli.

Alisema hata hivyo iwapo kuna mapungufu yaliyojitokeza yanaweza kurekebishwa kwa kuwa mradi upo hatua za mwanzo ambapo umefikia asilimia 10 tangu uanze kujengwa.

Warioba alibainisha kwamba mradi una thamani ya zaidi ya Sh. 1.67 bilioni unatarajia kuhudumia vijiji vine vya Itewe, Itaka, Hangomba na Bara  na kuwa umeanza kujengwa tanki lenye ujazo wa lita 150000 na unatarajia kuwanufaisha wakazi 32935 umeanza  mwezi Novemba mwaka huu na utakamilika Juni mwaka ujao.

Aidha naibu waziri Aweso alisema serikali ya awamu ya tano chini ya kampeni yake ya kumtua mama ndoo kichwani inawataka wataalamu na viongozi kutokuwa kikwazo cha kufanikisha kampeni hiyo badala yake watoke maofisini na kuhangaika kufanikisha azma hiyo.

Alisema wakati wa kutafuta vyanzo vya maji washirikishe wakazi wa maeneo husika kupitia mikutano ya hadhara ili kubaini uhaba halisi wa maji ili kuepuka migogoro inayoweza kujitokeza.

Awali Mbunge wa Jimbo la Mbozi Pascal Haonga alisema jimbo lake linakabiliwa na kero kubwa ya maji ambayo inasababisha ndoa kuvunjika na migogoro hivyo kuiomba serikali kutatua kero hiyo.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment