Social Icons

Wednesday, 27 March 2019

“Ligi ya Mabingwa wa Mikoa kituo cha Songwe Yapokelewa kwa Shangwe na Mashabiki”



Na Mwandishi Wetu, Mbozi

Mashabiki wa Soka katika mji wa Vwawa wilayani Mbozi mkoani Songwe wamesema  mashindano ya ligi ya Mabingwa wa mikoa kanda, yatawanufaisha kibiashara na kuwawezesha upya kuona mashindano makubwa baada ya timu ya Kimondo SC kushuka daraja miaka mitatu iliyopita.

Mmoja wa mashabiki wa mchezo wa soka wilayani hapa David Mwaibhofu alisema Songwe kupewa kituo cha mashindano hayo ni fursa kubwa ya kufanya biashara kwa kuwa wachezaji na baadhi ya mashabiki wao watakuwa wakipata huduma za kijamii zilizopo mkoani hapa hivyo kuongeza mzunguko wa fedha.

Alisema faida nyingine watakayoipata ni pamoja na kupata burudani ya mashindano makubwa waliyoikosa katika kipindi kirefu tangu kushuka kwa timu za Kimondo Sc na Karume Ranfers.
“uwanja mzuri tunao lakini hatuoni mashindano makubwa, hii ni changamoto kwa wadau wote wa michezo kushikamana ili kuwa na timu walau moja itakayoshiriki mashindano makubwa ya kitaifa”alisema David.

Naye Obadia Chilale alisema mashabiki wamefurahia kuanza kwa mashindano hayo kwani katika kipindi kirefu hawajapata burudani, lakini pia alieleza changamoto kwa chama cha mpira wa miguu mkoani hapa kuyatangaza zaidi ili wengi wafahamu na wapate nafasi ya kufika uwanjani kushuhudia timu zikimenyana.

Mmoja wa wachezaji wa Timu ya DTB Fc Juma A. Juma alisema mashindano hayo yatakuwa na ushindani mkubwa kutokana na kuwa kila timu iliyopo imekuja kwa lengo la kushinda na kusonga mbele katika hatua inayofuata.

“ timu zote zicheze mpira uwanjani zisitegemee mteremko maana kila mmoja amekuja kwa malengo yake ya kutaka kusonga mbele hakuna aliyekuja kwa lengo la kushindwa” alisema Juma

Kwa upande wake msemaji wa timu ya Nzihi Fc Jirani Hassan alisema licha ya timu yake kupoteza mchezo wa kwanza watajipanga vizuri ili kuhakikisha wanashinda michezo inayofuata.

Mashindano ya ligi ya mabingwa wa mikoa yaliyoanza jana katika vituo vinne hapa nchini na kukamilika April 11 mwaka huu ambapo timu 28 zinatarajia kumenyana vikari katika makundi hayo yatakayofanyika katika mikoa ya Simiyu, Katavi, Songwe, na Dodoma ambapo kila kundi litatoa washindi wawili ambao wataingia hatua ya nane bora ambayo washindi watatu wa juu watacheza ligi daraja  la pili Tanzania Bara.

Mwisho

No comments:

Post a Comment