Social Icons

Wednesday, 27 March 2019

Ligi ya Mabingwa wa Mikoa Yaanza Kituo cha Songwe


Na Mwandishi wetu

Timu ya Soka ya DTB FC toka Dar se salaam imeanza vizuri kusaka tiketi ya kuwania kufuzu katika  Ligi ya mabingwa wa mikoa katika kituo cha Songwe, baada ya kuichapa timu ya Nzihi FC Wanyalukolo toka Iringa kwa jumla ya mabao 2 – 1 katika mchezo wa ufunguzi uliochezwa katika uwanja wa CCM Vwawa wilayani Mbozi.

Mchezo huo ambao ulianza kwa kila timu kusoma mchezo wa mwenzake ambapo katika dakika 45 za kipindi cha kwanza  timu zote zilitoka suluhu bila kufungana.

DTB FC ndiyo ilikuwa ya kwanza kupata Bao la kwanza katika dakika 60 ya mchezo  lililofungwa na Dickson Samson, bao hilo lilidumu kwa muda wa dakika 17 baadaye kabla ya timu ya Nzishi Fc ya Iringa kupata bao la kusawazisha lililofungwa na Isaack Kivamba katika dakika ya 75 ya mchezo.

Hata hivyo kupatikana kwa baola kusawazisha kuliamsha ari ya wachezaji wa timu zote mbili kuanza kushambuliana kwa zamu na kuwa bahati ilikuwa ya DTB FC ambao walipata bao katika dakika 3  za nyongeza, hivyo hadi mwamuzi wa mchezo huo  Ahamad Kikumbo anapuliza kipenga cha kuashiria kumalizika dakika 90 za mchezo timu ya DTB FC ilikuwa mbele kwa mabao 2 – 1.

Kwa upande wake Kocha wa timu ya Nzihi Fc Edger Nzelu alisema vijana wake walicheza vizuri lakini kutokana na maamuzi mabovu ya mwamuzi na utelezi uwanjani uliosababishwa na mvua, wamepoteza mchezo huo hata hivyo alisema watajipanga vizuri katika machezo ujao ili kufanya vizuri zaidi.

Naye kocha wa timu ya DTB FC Kambi M. Kambi alisema timu pinzani muda wote walikuwa wakicheza mchezo wa kuotea ambao wachezaji wake walipoung’amua imesaidia kupata ushindi baada ya kutumia makosa ya wapinzani wao.

Kituo cha Songwe kina jumla ya timu 7 za DTB Fc Dar es salaam), Nzihi Fc (Iringa), Mpera Pesa (Songwe), makete United (Njombe), Top Boys (Ruvuma), Coast Star (Pwani) na Dipotivo Mang’ula (Morogoro) na kwamba mashindano hayo yanatarajia kuendelea kesho ambapo kutakuwa na michezo miwili itakayohusisha timu 4.

Mchezo wa kwanza utakaoanza saa 8 mchana utakuwa ni kati ya wenyeji Mpera Pesa na Dipotivo Mang’ula ya Morogoro na mchezo wa pili utakuwa kati ya Makete United ya Njombe na Top Boys ya Ruvuma, michezo yote itachezwa katika uwanja wa CCM Vwawa wilayani Mbozi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment