Social Icons

Friday, 29 March 2019

Waziri Mbarawa Awapa Matumaini Mapya ya Kupata Maji Wananchi


Na  Jonas Simbeye, Tunduma

Waziri wa maji Profesa Makame Mbarawa amekuja na matumaini kwa wakazi wa mkoa wa Songwe hususani miji ya Vwawa, Itumba Isongole na Tunduma ya kuwapatia maji safi na salama kufuatia Serikali kuwalipa madeni ya Makandarasi waliyokuwa wakiidai, na hivyo kufanya miradi hiyo kukwama na sasa itaendelea hadi kumalizika.

Alisema miradi mitatu mikubwa ya maji yenye thamani ya zaidi ya Sh. 3.2 bilioni katika wilaya tatu za mkoa wa Songwe, iliyokuwa imekwama kukamilika kwa sababu za ukosefu wa fedha inatarajia kukamilika  mwezi mmoja toka sasa na kuanza kutoa maji.

 Waziri Mbarawa alisema hayo  katika ziara yake ya kukagua miradi hiyo ambayo imekwama kutokana na ukosefu wa fedha na kuwa sasa Makandarasi hao wamelipwa fedha zao kilichobaki ni kuwasimamia  wamalize kazi walizopewa ili wananchi waanze kupata maji.

Alisema lengo la ziara yake ni kupita kwenye miradi yenye changamoto kubwa ambazo zimekwamisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya kumtua mwanamke ndoo kichwani.
Mbarawa aliitaja baadhi ya miradi mkoani Songwe yenye changamoto kuwa ni pamoja na mradi wa maji Vwawa, Itumba – Isongole, Tunduma na mradi wa maji Tindingoma katika halmashauri ya wilaya ya Momba ambao alizuia fedha ili ajiridhishe kwa kuutembelea ndipo fedha zitolewe.

Awali Mkuu wa mkoa wa Songwe Brigedia Jenerali Mstaafu Nicodemas Mwangela akizungumza wakati wa kutoa taarifa yab hali ya maji mkoani hapa ambayo ni asilimia 46.3 katika maeneo ya vijijini na aslimia 40.8 kwenye maeneo ya mjini na kuwa na wastani wa jumla wa upatikanaji wa huduma ya maji mkoani hapa kuwa asilimia 45.3.

Alisema pia mkoa unakabiliwa na changamoto ya Makandarasi kutolipwa fedha zao kwa wakati hali inayofanya miradi ya maji kutokamilika kwa wakati, ambapo miradi hiyo ilipaswa iwe imekamilika tangu Desemba 31 mwaka juzi lakini kutokana na sababu hiyo ililazimika kuongeza muda.

Kwa upande wake Mhandisi wa maji Mamlaka ya maji na usafi wa mazingira Mbeya Ndele Mengo alifafanua kuwa mradi wa maji Vwawa  umefikia kiwango cha asilimia 90 ili ukamilike, Itumba Isongole asilimia 84 na Tunduma asilimia 96 na kwamba miradi hiyo imesalia kazi ndogondogo za umaliziaji. 

Mkandarasi anayejenga mradi wa maji Itumba Isongole wilayani Ileje toka kampuni ya Singirimu Enterprises Abdala Digelo alieleza sababu za kushindwa kukamilika kwa mradi huo kuwa ni pamoja na kushindwa kufikisha vifaa eneo la ujenzi kutokana na mvua kunyesha na baadhi ya vifaa kutopatikana kwa wauzaji.

Naye Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Leo start engeneering  Johanes Mgosi inayojenga mradi maji Vwawa  Johanes Mgosi alieleza sababu za kuchelewa kwa mradi huo kuwa ni pamoja na ukosefu wa fedha na kuwa alithibitisha mradi huo kukamilika baada ya wiki mbili toka sasa baada ya kuwasili Pump aliyoiagiza na kisha kuanza kufanya kazi ya kufunga mita kwa watumia maji.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbozi John Palingo alisema wilaya yake imeandika andiko la mradi mkubwa wa maji wa kutosha vijiji 12 ambao upo Wizarani iwapo ukikamilika utasaidia kupunguza uhaba wa maji hadi kufikia asilimia zaidi ya 90 hivyo kumuomba Waziri asaidie.
Mwisho


No comments:

Post a Comment